
Wizara ya Afya Tanzania
February 11, 2025 at 07:49 PM
Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wadau wa Sekta Taasisi ya Village Reach pamoja na Taasisi ya ‘Center for International Health Education and Biosecurity (CIHEB) wanatarajia kuanza utekelezaji wa mradi wa kuimarisha afua mbalimbali za huduma za Dharura wakati wa magonjwa ya Mlipuko
Hayo yamebainishwa kwenye kikao kilichowakutanisha Dkt.Erasto Sylvanus Kaimu Mkurugenzi wa huduma za Dharura na Maafa kutoka Wizara ya Afya, pamoja na watendaji kutoka Taasisi hizo kwenye mkutano uliofanyika katika Ofisi za Wizara, Jijini Dodoma Februari 11, 2025 kuhusu utekelezaji wa mradi huo.
“Lengo la mradi huu ni kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya kuhusu afua za kukabiliana na magonjwa ya mlipuko na kuimarisha ugavi wa dawa na vifaa muhimu, na kuimarisha huduma za usaidizi wakati wa milipuko ya magonjwa, ” amebainisha Dkt. Sylvanus.
Amesema kuwa mradi huo utasaidia kuimarisha usafirishaji wa sampuli za magonjwa ya mlipuko kwa wakati na ufanisi kutoka vituo mbalimbali vya kutolea huduma za afya kwenda maabara za uchunguzi.
Mradi unatarajiwa kuboresha kwa kiasi kikubwa uwezo wa nchi wa kusimamia na kukabiliana na dharura za afya, kuimarisha utayari wa jumla wa kukabiliana na majanga na kuhakikisha ufuatiliaji bora zaidi wakati wa milipuko ya siku zijazo.
Mradi huu unatarajiwa kutekelezwa ndani ya kipindi cha miaka miwili na umefadhiliwa na Shirika la Takeda la nchini Japan kupitia taasisi ya village Reach iliyowakilishwa na
Bi. Wema Kamuzora na kutekelezwa na Taasisi ya Center for International Health Education and Biosecurity (CIHEB)- Tanzania inayoongwa na Dkt. Abubakar Maghimbi Mkurugenzi wa Taasisi hiyo.
👍
👏
😂
3