
MEFTAHUL 'ULUUM 📚🔑📚
May 23, 2025 at 09:49 PM
SHAIRI: SEMA NAYE
Mtunzi: Tulaybu
1.Naukunjua mkeka, njoo tushauriane
Dada yangu pia kaka, nasaha tuambiane
Kamwe tusifuge taka, vema tunasihiane
Mapema useme naye, singoje muda upite
2.Sema na wako mtoto, mapema angali chini
Ni baridi au joto, mfunze awe makini
Awe Kurwa au Doto, mpe maneno laini
Mapema useme naye, singoje muda upite
3.Mpe elimu kijana, elimu ya maadili
Ya leo sio ya jana, azitulize akili
Sema bila kuyabana, yasimzonge maswali
Mapema useme naye, singoje muda upite
4.Watoto lao hitaji, wayafikie malengo
Hivyo kwenye ukuaji, usiwaachie pengo
Wasiwe wazururaji, maisha ya songombingo
Mapema useme naye, singoje muda upite
5.Hali imeshachafuka, kwa wakike na kiume
Watoto wahitajika, maadili wayasome
Sio usiku kuruka, mithili ya paka chume
Mpema useme naye, singoje muda upite
6.Mjengee marafiki, wema wasio waovu
Sio wale wanafiki, mwanao mpe makavu
Muonye kama hataki, kwa upole utulivu
Mapema useme naye, singoje muda upite
7.Ukae naye karibu, mfanye wako swahiba
Umzoeshe vitabu, hwena akaleta toba
Atazijua adhabu, maovu akiyabeba
Mapema useme naye, singoje muda upite
_____________________
Sat, 24 May 2025
Tulaybu ✍️ 0714388284

👍
1