
WIZARA YA MAMBO YA NJE
162.9K subscribers
Verified ChannelAbout WIZARA YA MAMBO YA NJE
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Tanzania _______________________________________________ Tanzania Ministry of Foreign Affairs and East African Cooperation
Similar Channels
Swipe to see more
Posts

RAIS MSTAAFU WA AFRIKA YA KUSINI MHE. THABO MBEKI AWASILI NCHINI KUSHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA AFRIKA Rais Mstaafu wa Afrika ya Kusini Mhe. Thabo Mbeki amewasili nchini Tanzania Mei 20, 2025, kushiriki Mhadhara wa Siku ya Afrika (Africa Day Lecture) ulioandaliwa na Taasisi ya Thabo Mbeki kwa ushirikiano na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambao utafanyika jijini Dar es Salaam tarehe 24 Mei, 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Mhe. Thabo Mbeki amepokelewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato David Chumi (Mb.). Mhadhara huo ambao ni wa 15 kuandaliwa na Taasisi ya Thabo Mbeki, unatarajiwa kujadili kuhusu mustakabali wa Bara la Afrika na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wakiwemo wanataaluma, wadau kutoka Serikalini, viongozi wastaafu, vijana, na wawakilishi wa sekta binafsi. Sambamba na Mhadhara huo, Mhe. Rais Mstaafu Mbeki anatarajiwa kushiriki katika mijadala mbalimbali ikiwemo; mjadala kuhusu Uchumi wa Buluu na Utalii, mjadala wa Wanataaluma wa Vyuo Vikuu, halikadhalika majadiliano kuhusu Fursa ya Urais wa Afrika ya Kusini wa kundi la Nchi zenye Uchumi Mkubwa Duniani (G20) kwa ustawi na maendeleo ya Afrika. Mhadhara wa Siku ya Afrika unafanyika nchini baada ya Taasisi ya Thabo Mbeki kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji kwa ukanda wa Afrika Mashariki.


TANZANIA NA FINLAND KUSHIRIKIANA KATIKA DIPLOMASIA YA UCHUMI Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Finland zimeazimia kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kupitia sekta za kimkakati kama vile nishati, biashara na uwekezaji, ili kukuza diplomasia ya uchumi. Azma hiyo imefikiwa katika kikao cha pamoja kilichofanyika katika Ofisi Ndogo ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jijini Dar es Salaam, kikihusisha viongozi waandamizi kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Naibu Waziri wa Biashara za Kimataifa wa Finland, Mhe. Jarno Syrjälä. Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa, amesema Tanzania inaendelea kuimarisha diplomasia ya uchumi kwa kushirikiana na mataifa rafiki kama Finland, kwa lengo la kufungua fursa zaidi za maendeleo. Amesisitiza kuwa ushirikiano huo una mchango mkubwa katika kuleta teknolojia, mitaji, na ujuzi unaoweza kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa. Kwa upande wake, Mhe. Syrjälä amepongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia wawekezaji wa kimataifa. Amesema Finland iko tayari kushirikiana na Tanzania katika maeneo yenye maslahi kwa pande zote, hususan nishati jadidifu, teknolojia ya kisasa na elimu ya ufundi stadi. Katika kikao hicho, ujumbe wa Tanzania uliwasilisha vipaumbele vya Serikali katika kukuza uchumi kupitia sekta ya viwanda, kilimo, nishati na utalii. Pia, ujumbe huo umetoa wito kwa wawekezaji kutoka Finland kutumia fursa zilizopo kuwekeza nchini. Ujumbe wa Tanzania katika kikao hicho ulijumuisha viongozi na wataalam kutoka Wizara ya Nishati, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Kilimo pamoja na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC).


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amempokea Rais wa Jamhuri ya Namibia, Mheshimiwa Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah Ikulu, jijini Dar es Salaam, Mei 20, 2025.


Matukio mbalimbali ya Uzinduzi wa Baraza jipya la Wafanyakazi la Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa JNICC, uliopo jijini Dar es Salaam. Tukio hilo limefanyika tarehe 11 Mei, 2025.

Rais wa Jamhuri ya Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah amewasili nchini Mei 20, 2025 kwa ajili ya kuanza ziara rasmi ya siku mbili kuanzia tarehe 20 hadi 21 Mei, 2025. Ziara hiyo ya kwanza kwa Mhe. Nandi-Ndaitwah kufanyika hapa nchini tangu kuingia kwake madarakani mwezi Machi 2025, inafuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, Mhe. Dkt. Nandi-Ndaitwah amepokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo. Akiwa nchini pamoja na mambo mengine, Mhe. Dkt. Nandi-Ndaitwah atafanya mazungumzo ya faragha na mwenyeji wake, Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan yatakayofuatiwa na mazungumzo rasmi ya kujadili namna ya kukuza ushirikiano baina ya nchi hizi mbili. Kadhalika Viongozi hao kwa pamoja watazungumza na Waandishi wa Habari kuelezea makubaliano waliyofikia katika mazungumzo yao kabla ya kushiriki dhifa ya chakula cha jioni iliyoandaliwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa heshima ya Mhe. Dkt. Nandi-Ndaitwah. Akiendelea na ziara yake nchini, Mhe. Rais Dkt. Nandi-Ndaitwah, Mei 21, 2025 anatarajiwa kutoa Mhadhara katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam pamoja na kutembelea Kituo cha Urithi wa Ukombozi wa Afrika kilichopo Dar es Salaam. Tanzania na Namibia zimeendelea kuimarisha ushirikiano wa kihistoria ulioasisiwa na Waasisi wa mataifa haya mawili Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Sam Nujoma kupitia mikataba mbalimbali ya uwili na masuala yote yanayohusu Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).


Leo tarehe 20 Mei, 2025, Mhe. Cosato Chumi (Mb.), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Italia nchini, Mhe. Giuseppe Coppola. Mazungumzo hayo yamefanyika katika Ofisi za Wizara jijini Dar es Salaam. Katika mazungumzo hayo, Mhe. Balozi Coppola ameeleza kuhusu nia ya Serikali ya Italia kuendelea kuunga mkono jitihada za kuleta maendeleo zinazofanywa na Serikali chini ya uongozi mahiri wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika kuthibitisha hilo, Balozi Coppola amejulisha kuwa Italia iko katika hatua za mwisho za kukamilisha mkopo wa gharama nafuu wa Dola milioni 281 kusaidia utekelezaji wa Awamu ya nne ya Ujenzi wa Reli ya Kisasa. Vilevile, alijulisha kuhusu kurejeshwa kwa Tanzania katika orodha ya nchi zinazonufaika na mitaji inayowezesha kuboresha elimu ya ufundi stadi, ambapo kupitia mpango huo Tanzania itanufaika na ufadhili wa hadi Euro milioni 20. Katika hatua nyingine, Tanzania na Italia zilikubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uchumi wa buluu, uchukuzi na usafirishaji, mawasiliano na teknolojia ya habari, kilimo na ufugaji, ulinzi na usalama pamoja na biashara na uwekezaji.

Leo tarehe 20 Mei, 2025, Mhe. Cosato Chumi (Mb.), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Italia nchini, Mhe. Giuseppe Coppola. Mazungumzo hayo yamefanyika katika Ofisi za Wizara jijini Dar es Salaam. Katika mazungumzo hayo, Mhe. Balozi Coppola ameeleza kuhusu nia ya Serikali ya Italia kuendelea kuunga mkono jitihada za kuleta maendeleo zinazofanywa na Serikali chini ya uongozi mahiri wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katika kuthibitisha hilo, Balozi Coppola amejulisha kuwa Italia iko katika hatua za mwisho za kukamilisha mkopo wa gharama nafuu wa Dola milioni 281 kusaidia utekelezaji wa Awamu ya nne ya Ujenzi wa Reli ya Kisasa. Vilevile, alijulisha kuhusu kurejeshwa kwa Tanzania katika orodha ya nchi zinazonufaika na mitaji inayowezesha kuboresha elimu ya ufundi stadi, ambapo kupitia mpango huo Tanzania itanufaika na ufadhili wa hadi Euro milioni 20. Katika hatua nyingine, Tanzania na Italia zilikubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta ya uchumi wa buluu, uchukuzi na usafirishaji, mawasiliano na teknolojia ya habari, kilimo na ufugaji, ulinzi na usalama pamoja na biashara na uwekezaji.

FINLAND YAKARIBISHWA KUWEKEZA KATIKA MIRADI YA MAWASILIANO NCHINI Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesisitiza dhamira yake ya kuimarisha ushirikiano na Serikali ya Finland katika sekta ya mawasiliano kwa lengo la kukuza teknolojia na kuendeleza miundombinu ya kisasa nchini. Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo, wakati wa kikao na Naibu Waziri wa Biashara za Kimataifa wa Finland, Mhe. Jarno Syrjälä, kilichofanyika katika ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam. Balozi Shelukindo ameeleza kuwa Tanzania inatambua nafasi muhimu ya sekta ya mawasiliano katika kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Amesisitiza kuwa Serikali ipo tayari kushirikiana na wawekezaji kutoka Finland, hususan kampuni zilizobobea katika teknolojia ya mawasiliano kama Nokia, ili kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma za mawasiliano nchini. “Tunaamini kuwa ushirikiano wa kimkakati katika sekta ya mawasiliano utasaidia kuongeza tija katika sekta za biashara, elimu, na huduma za kijamii,” alisema Balozi Shelukindo. Akiwa amembatana na ujumbe wa wawakilishi wa sekta binafsi kutoka Finland, wakiwemo wawakilishi wa Kampuni ya Nokia, Mhe. Syrjälä ameeleza kuwa Finland imejipanga kuimarisha ushirikiano na Tanzania katika maeneo ya maendeleo. Amebainisha kuwa kampuni za teknolojia kutoka Finland, ikiwemo Nokia, zipo tayari kushiriki katika utekelezaji wa miradi ya mawasiliano nchini. Mazungumzo hayo yamehudhuriwa pia na wawakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa , Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji pamoja na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), ambao wameeleza utayari wa kushirikiana na Finland katika kukuza sekta ya mawasiliano kama kichocheo cha maendeleo endelevu.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mjumbe maalum, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) amewasili jijini Kampala Uganda na kupokelewa na Balozi wa Tanzania nchini Uganda Mhe. Maj. Gen. Paul K Simuli katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe tarehe 12 Mei, 2025. Waziri Kombo anatarajiwa kuwasilisha Ujumbe maalumu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Gen. Yoweri Kaguta Museveni.
