
UFUNUO CHANNEL
194 subscribers
About UFUNUO CHANNEL
Karibu UFUNUO CHANNEL tunakusogezea mafundisho ya unabii kila wiki, pamoja na mafundisho mbalimbali katika biblia. Tufuatilie kwenye mitandao mingine ya kijamii Twitter au X: x.com/ufunuochannel Instagram: instagram.com/ufunuochannel Youtube: youtube.com/ufunuochannel
Similar Channels
Swipe to see more
Posts

_Nami nikawaona wale malaika saba wasimamao mbele za Mungu, nao wakapewa baragumu saba. Ufunuo 8:2_ Katika kuonesha hatua za Mungu za kuingilia kati kwa niaba ya watu Wake, Ufunuo hutumia vielelezo vya tarumbeta katika Agano la Kale. Tarumbeta vilikuwa vyombo muhimu vya maisha ya kila siku ya Israeli ya zamani (angalia Hes. 10:8–10 , 2 Nyak. 13:14, 15). Sauti zake ziliwakumbusha watu juu ya ibada hekaluni; tarumbeta zilipulizwa pia katika vita, wakati wa mavuno, na wakati wa sikukuu. Upulizaji wa tarumbeta uliambatana na maombi. Wakati wa ibada hekaluni au wakati wa sikukuu, tarumbeta “zilimkumbusha” Mungu juu ya agano Lake na watu Wake. Pia ziliwakumbusha watu wawe tayari kwa ajili ya “siku ya Bwana” (Yoeli 2:1). Wakati wa vita, sauti ya tarumbeta, iliyoambatana na maombi, ilimwita Mungu awaokoe watu Wake. Dhana hii ni msingi wa tarumbeta katika Ufunuo. Tukio lililoashiriwa kwa tarumbeta katika Ufunuo hudokeza juu ya hatua ya Mungu ya kuingilia kati katika historia kama jibu la maombi ya watu Wake. Wakati ambapo kimsingi muhuri unawahusu wale wanaodai kuwa watu wa Mungu, tarumbeta hutangaza hukumu dhidi ya wakazi wa dunia (Ufu. 8:13). Wakati huohuo, haya ni maonyo kwa watu ili kuwaleta katika toba kabla hawajachelewa kabisa. Tarumbeta saba hukamilisha historia nzima tangu wakati wa Yohana hadi hitimisho la historia ya dunia hii (Ufu. 11:15–18). Zinapulizwa ilhali maombezi yakiendelea mbinguni (Ufu. 8:3–6), na injili ikihubiriwa duniani (Ufu. 10:8–11:14). Hukumu za tarumbeta hizi ni kwa sehemu tu; huathiri theluthi tu ya uumbaji. Tarumbeta ya saba hutangaza kwamba muda umewadia kwa ajili ya Mungu kutwaa utawala Wake stahiki. Tarumbeta saba zinahusika takriban katika vipindi husika vinavyohusika na makanisa saba: Tarumbeta mbili za kwanza hutangaza hukumu juu ya mataifa yaliyomsulubisha Kristo na kulitesa kanisa la awali, Yerusalemu mwasi, na Himaya ya Rumi. Tarumbeta ya tatu na ya nne huonesha mwitikio wa mbingu kwa uasi wa kipindi cha zama za kati na baada ya Matengenezo. Tarumbeta ya tano na ya sita huelezea hali katika ulimwengu wa kipagani baada ya Zama za Maarifa, zinazobainishwa kwa utendaji mkubwa wa nguvu za kishetani zinazoukusanya ulimwengu kwenye vita vya Har-Magedoni.

_Nikasikia hesabu yao waliotiwa muhuri katika kila kabila ya Waisraeli, watu mia na arobaini na nne elfu. - Ufunuo 7:4_ Tangazo la idadi ya wale waliotiwa muhuri linaashiria ukamilishwaji wa hatua hiyo. Yohana anasikia kwamba idadi yao ni 144,000 kutoka katika makabila 12 ya Israeli. Rejea hii haihusu tarakimu halisi bali kile inachoashiria. Tarakimu hii (144,000) inaundwa 12 mara 12 mara 1,000. Kumi na mbili ni ishara ya watu wa Mungu: makabila ya Israeli na alama ya kanisa likiwa limejengwa juu ya msingi wa mitume 12 (Efe. 2:20). Hivyo, tarakimu 144,000 huwakilisha utimilifu wa watu wa Mungu wa siku za mwisho, udhihirisho wa kisasa wa Israeli ya zamani. Makabila 12 yaliyoorodheshwa katika Ufunuo 7 si ya kihistoria, kwa sababu makabila 12 ya Israeli hayapo leo. Makabila 10 yalichukuliwa utumwani wakati wa shambulio la Waashuri (2 Wafalme 17:6–23), ambapo walichangamana na mataifa mengine. Makabila 12 hayaundi dini ya Kiyahudi leo. Orodha ya makabila 12 ya Ufunuo 7 si orodha yenye mpangilio wa kawaida. Yuda anaorodheshwa kama kabila la kwanza badala ya Reubeni. Pia, makabila ya Dani na Efraimu yameondolewa, na Yusufu na Lawi yamejumuishwa badala yao. Sababu bayana ya kuondolewa kwa Dani na Efraimu ni kwa vile katika Agano la Kale makabila mawili haya ni waasi na waabudu-sanamu (Amu. 18:27–32, Hos. 4:17). Orodha ya makabila katika Ufunuo 7 si ya kihistoria bali kiroho. Hutuambia kwamba ukosefu wa uaminifu kwa makabila ya Dani na Efraimu hauna nafasi miongoni mwa watu wa Mungu waliotiwa muhuri. Pia, kanisa katika Agano Jipya hutajwa kama makabila 12 ya Israeli (Yakobo 1:1). Makabila 12 katika Ufunuo 7 huwakilisha watu wa Mungu wote, Wayahudi na Wamataifa. Hawa 144,000 wanaoneshwa kama jeshi lililoundwa kwa mfumo wa Israeli ya zamani wakienda vitani. Katika Israeli ya zamani, palikuwa na askari 1,000 katika kombania moja ya jeshi (Hes. 31:3–6). Namba 144,000 ya ishara huonesha kanisa lililoko vitani kwa namna ya kombania 144 za kijeshi zenye askari 1,000 waliotayari kwa ajili ya vita vya mwisho (Ufu. 17:14), tofauti na jeshi la adui lenye idadi ya milioni 200 (Ufu. 9:16).

_Nikaona malaika mwingine, akipanda kutoka maawio ya jua, akiwa na mhuri wa Mungu aliye hai... Ufunuo 7:2_ Katika Agano la Kale, pepo husimama badala ya nguvu angamizi azitumiazo Mungu ili kutekelezea hukumu juu ya waovu (Yer. 23:19, 20). Ni njia nyingine ya kuelezea mapigo saba ya mwisho yatakayomimiwa juu ya wanadamu wasiotubu mara tu kabla ya Marejeo (Ufunuo 16). Hata hivyo, nguvu hizi angamizi zinazuiwa kwa Mungu kuingilia kati wakati hatua ya kuwatia muhuri watu wa Mungu ikifanyika. Katika nyakati za zamani, maana ya msingi ya kutiwa muhuri ilikuwa umiliki. Maana ya kutiwa muhuri kiishara katika Agano Jipya ni kwamba “Bwana awajua walio wake” (2 Tim. 2:19). Mungu huwatambua watu Wake na kuwatia muhuri kwa Roho Mtakatifu (Efe. 1:13, 14; 4:30). Katika wakati wa mwisho, muhuri katika kipaji cha uso huwabainisha wale wanaochagua kuwa upande wa Mungu (Ufu. 14:1). Muhuri wa Mungu si alama inayoonekana iwekwayo kwenye kipaji cha uso wa mtu, bali humaanisha “kutulia katika kweli, kiakili na kiroho, kiasi kwamba hawawezi kuhamishwa.” Wale ambao, kwa kujua na kuridhia, wanajiunga na mnyama hupokea chapa ya mnyama (Ufu. 13:16, 17). Uaminifu wa watu wa Mungu waliotiwa muhuri umepimwa katika kila kizazi. Hata hivyo, kipimo cha uaminifu katika zahama ya mwisho kitakuwa utunzaji wa amri za Mungu (angalia Ufu. 12:17, 14:12).