MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ WhatsApp Channel

MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ

664 subscribers

About MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ

MAJIVU YA FASIHI ✍🏿 Ni kituo kinachokuletea burudani na elimu kupitia fasihi andishi. Karibu tufurahie; 1. Visa na hadithi πŸ“– 2.RiwayaπŸ“š 3.Uchambuzi wa filamu🎬🎞 4.Makala mbalimbali (Michezo, Sayansi na maisha)πŸ“ƒ Vyote katika lugha adhimu ya kiswahili... @Kalamu_ya_kabati @Chivihi's son

Similar Channels

Swipe to see more

Posts

MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
6/2/2025, 8:56:08 PM

RIWAYA; *KIBIRITINGOMA* MTUNZI; *GODLOVE KABATI* KWENDA KWA; *MAJIVU YA FASIHI channel* WhatsApp; 0763204351 ----------------- SEHEMU YA KUMI NA MOJA *Mwanaume mnyime ugali...atakula hata viazi.* *Mnyime kanzu, atavaa hata kaniki mbovu ama gunia* *Mnyime salamu, hii ataipata popote pale kwingineko kama sio kwako.* *Lakini chondechonde, katu usimnyime heshima yake.* *Na hii ni sehemu ya kumi na moja.* Siku yake iliyoanza kwa bashasha sasa ilikuwa imegeuka siku mbaya. "Siku ya shetani hii!" Nafsi yake ilimshtakia, kila alipolinganisha vibwanga na vibweka vyote vilivyomuandama siku hii. Didas Ambrozi alikuwa njiani kuelekea asikokujua. Alikuwa amechanganyikiwa haswaa. Mikono yake ilioshikilia usukani ilikuwa bado inamtetemeka kwa hasira. Kila mara jina la Bebe likimjia kichwani ana sonya na kutukana kimoyomoyo. Mara nyingine anapiga honi hovyohovyo kwa kuupiga kwa nguvu usukani. "Nimeyaona macho yake yule mnafiki. Changudoa mkubwa na tapeli kutoka kuzimu. Nimeyaona macho yake, yalikuwa makavu kabisaaa. Malaya yule!" Hatimaye akatamka kwa sauti akilalamika. Sentensi zake zikafuatiwa na honi iliyomkurupua mwendesha baiskeli ambaye aliponea chupuchupu kupitiwa na gari lile lililokuwa kasi. Didas amechachamaa! "Machozi yake ni ya kinafiki! Machozi ya wizi kabisa. Nimemuona usoni! Msaliti...mpumbavu." Didas akazidi kulalamika, akatema mate kwa hasira, amesahau kuwa yu ndani ya gari lake zuri la kifahari. "Yaani jitu pumbavu pumbavu litoke huko kusikojulikana, lile magimbi na ugali lisishibe...halafu liniamrishe eti ooh, nipe milioni mia halafu sitisha mkataba! Mimi huyooo?! Yeye kama nani kwanza." Didas yu peke yake garini, bado analalamika. Safari hii ghafla akashika breki zake kwa nguvu almanusura amgonge mlemavu aliyekuwa anavuka barabara kwenye alama za pundamilia. Nje ya gari, aliweza kuwatazama watembea kwa miguu waliokuwa wamecharuka kwa hasira, ndita zimechoreka kwenye nyuso zao, midomo na vinywa vyao vikionekana kumnenea maneno ya hasira kwa kuaalamika. Vidole vyao vya shahada vikilinyookea gari lake la kifahari lililomficha kwa vioo vyeusi vyenye sifa ya 'Wa ndani anamuona wa nje, lakini huyu wa nje katu, hawezi kuona kilicho ndani.' Yeye hakuwasikia na akamshukuru sana yule mtu mwerevu aliyebuni vioo vya namna ile. Mzee yule mlemavu alipovuka salama, akachochea upya gari lake na kufyatuka eneo lile. Baada ya kilomita chache akagundua kuwa anakosa umakini kwenye kuendesha gari. Akaliegesha gari lake kando ya barabara na kutulia akijipa dakika chache ili afanye tafakuri. Bado mawazo yake yanashindwa kuamini kuwa huenda Bebe amemzunguka na kumchezea shere tena katika namna ya kitapeli. "Au namsingizia?" Akajihoji. "Hapana simsingizii!" Akajijibu. "Hawa malaya wana mambo mengi sana ya ovyo! Wana mitandao yao ya siri ya kufanya uhalifu na dhambi zote zimchukizazo muumba." Sasa Didas akaikumbuka kofia yake ya uzee wa kanisa. "Yaani afanye uzinifu na uasherati huko halafu nimpe-" Mawazo yake yakavurugwa na mlio wa simu yake iliyoita kwa ghafla. Akaitazama kwa hofu, nambari iliyokuwa imempigia wakati huu ilionyesha kuwa ya tofauti kidogo. Akaitazama kwa sekunde chache. Kumbukumbu zake zikamkumbusha kuwa aliwahi kuziona mahali. Namba za namna hii hutumiwa na watu wachache sana hasa wale walio kwenye sekta nyeti za kiserikali kama mawaziri au usalama wa taifa. "Atakuwa nani huyu ambaye sijamsevu?" Didas akaingiwa na hofu akiinua simu yake tayari kwa kuipokea. Alikuwa akifahamiana na viongozi wengi tu wakubwa wa kiserikali, lakini wote alikuwa na mawasiliano nao. Ni kwa namna gani simu hii mpya imjie tena kwenye nyakati kama hizi ambazo anaandamwa na hofu? "Video zimewafikia!!" Kengele ya hatari ikalia kwenye ubongo wake. Akaketi vizuri na kujikohoza ili kuweka sawa sauti yake kisha akaipokea simu ile kwa nidhamu na unyenyekevu mkubwa. "Ha...haloo!" "Naongea na Didas Kilonzo Ambrozi!" Sauti nzito changamfu iliyoonekana kuwa na haraka ilipepea kutoka kwa mpigaji. Didas akagutuka. Kutajwa kwa majina yake matatu kama yalivyo kwenye vyeti vyake vya elimu, kukamshtua. Tena wakati huu hakuitwa bwana au muheshimiwa. Hakika alikuwa anaongea na mtu mkubwa. "Naam ni..ni mimi!" Akajibu kwa kigugumizi. "Unaongea na Special agent YW536 kutoka kitengo cha kiintelijensia na usalama wa mitandao Tanzania." Utambulisho huu ukamfanya Didas apate tumbo la kuhara. Akajishikilia kwa nguvu ili kujizuia. Mfano wa vitu kama vipepeo, vinapepea tumboni mwake. "Kwa nini unafanya mambo ya aibu ndugu yangu?" Swali jepesi la kiungwana lakini linalotatanisha likaachika kutoka kwa mpigaji yule. Mfumo wa upumuaji wa Didas ukabadilika. Pumzi zikaanza kupishana kwa kasi puani mwake, hakujua ajibu nini. Maadamu anayeongea naye ni mtu wa ndani ya mfumo, basi kuna uhakika wa asilimia zote kuwa ameziona video zake. Hakuwa na sababu yoyote ya kupoteza muda kuuliza mambo gani ya aibu aliyoyafanya. Aulize ili atumbuliwe? "Nisaidie ndugu yangu!" Kauli hii ikamtoka kwa uchungu huku akiikumbatia simu ile kwa mikono yote miwili sikioni mwake. Alikuwa anazungumza na masihi wake. "Hapa nakusaidiaje Didas? Enhe? Yaani ungejua namna unavyoheshimika huku lkulu, sidhani kama ungefanya huu upuuzi wa kujirekodi ukifanya uchafu. Huu ni upuuzi aisee! Akiona mheshimiwa Raisi itakuweje? Kwenye mitambo hapa inaonesha bado nusu saa, video zote ishirini zitakuwa mitandaoni! Na mtandao wa kwanza kufikiwa na huu upuuzi ni ule unaotumiwa na serikali." Sauti ya mpigaji ikapandwa na jazba, bado kasi yake ni ya haraka na haina mahusiano na utani wa aina yoyote ile. Yalipotajwa maneno kama *Raisi* na *serikali* , ushuzi ulimponyoka Didas kwa mafungu. "Bwana mkubwa! Bwana mkubwa! Naomba unisaidie kaka. Ni wahuni tu wamenifanyia mchezo mchafu. Nimeangushiwa jumba bovu ndugu yangu!" Ni Didas kwenyw harakati za kuutafuta wokovu wake. "Mimi sio ndugu yako! Na wala usiniite kaka. Sina undugu na wazee wazinifu wasio na uaminifu kwa wake zao. Wewe mzee hauna maadili kabisa!" Sauti ile inaonekana kama haitaki kupoteza muda, ni nzito, sauti ya mamlaka. "Kesi za maudhui ya namna hii hutufikia siye kabla ya kuingia mitandaoni. Yapo yanayofutika na yapo maudhui kama haya tusiyoweza kuyafuta kutokana na umahiri na ujanja wa mdukuzi anayeyapakia kwenye system. Na mimi siko tayari kuona huu uchafu unaingia kwenye rada za serikali yetu tukufu ya Jamhuri. Kwanza ni bahati sana nimeipata namba yako na nikakupigia. Nimekuheshimu sana kwa vile mimi ni mpenzi wa bidhaa za kampuni yako. Kimsingi sina cha kukusaidia, Lakini kama kuna mtu unayedaiana naye kwa namna yoyote ile, mlipe kabla ya nusu saa... Ama sivyo, Mzee wangu...jiandae kisaikolojia! Adui yako anaijua teknolojia vyema kuliko kitu chochote kile!" Simu ikakatwa. Upesi! Didas hakuwa na muda wa kujiuliza mara mbili. Akaliwasha gari lake na kuugeuza usukani. Gari likachomoka kwa kasi kuelekea eneo lolote lile ambalo alifahamu kuwa kuna jengo linaloitwa benki. Kiburi na majivuno yake yote akaamua avitie mfukoni kwa muda. Shilingi yake ya ukombozi ilikuwa ikinesanesa kiganjani mwake karibu na tundu la choo, hakutaka kuipoteza! Potelea mbali kama Bebe ni msaliti, mnafiki ama malaika mtoa roho. Akampigia simu mara moja kutaka kukutana naye ofisini mwake. Alikuwa ni kama aliyepewa mzani achague ni kipi chenye uzito kati ya utajiri na heshima yake alivyovihangaikia tangu zamani akiwa kijana, ama msichana changudoa aliyekutana naye ukubwani na kuamua kumsaidia. Wakati huu akaipa heshima yake uzito wa jiwe la fatuma mbele ya Bebe mwenye uzito wa unyoya. ******** "Saini hapa na hapa!" Didas anaitazama saa yake, upara wake unavuja jasho. Anamtazama Bebe ambaye naye ni kama haelewi ni nini kinachoendelea. "Nisaini nini tena mbona sielewi?" Bebe anauliza. "Usinichanganye! We saini hapa... sina muda wa kupoteza. Mengine utayajua mbele ya safari." Didas anabwata, matone kadhaa ya mate yakimtoka kinywani. Tai yake shingoni imegeuka nyuma. Ina maana kifua chake kimehamia mgongoni?Hatujui. Anajua yeye. Bebe akakamata kalamu ile ya wino na kuanza kusoma karatasi ile kabla hajasaini. "Come on! Unasoma nini tena?" "Unataka nisaini kitu ambacho sikijui? Kama unataka kuniuza?" Bebe akauliza kwa kujiamini. Didas akashusha pumzi kwa nguvu. "Sikia Frola!" Kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu akamtaja kwa jina lake halisi. "Hapa tunaongelea uhai na kifo! Heshima yangu na familia yangu niliyo nayo ni maisha yangu Frola. Huu ni mkataba wa kusitisha kazi yako wewe na kampuni yetu kama anavyohitaji huyo mwenzio...Ahhh (Anabadili) huyo jamaa aliyeturekodi. Umenielewa?!" Uso wake umetota kwa jasho anamtazama Bebe. "Ina maana naacha kazi?" "Yeah! Haya saini hapa." "Kwa nini lakini?" "Bebe...hayo masuala mengine tutajua baadae. Tazama! Tuna dakika kumi na moja tu hapa." Bebe akaiinamia karatasi ile na kuanza kuchonga herufi zake. Didas anamtazama kwa shauku, bado anaona Bebe kama anaandika taratibu. Bebe akamaliza kutia saini yake. Didas akaikwapua bahasha kubwa ya kaki iliyosheni fedha kutoka kwenye begi dogo na kumkabidhi Bebe. "Haya mama! Mpelekee huyu jamaa hivi vitu haraka kwenye eneo nililokuelekeza. Fanya upesi." Didas akamsurutisha Bebe. "Lakini-" "We nenda, hili likiisha hayo mengine tutayaongea!" Didas akamkatisha. Bebe akaondoka kishingo upande kutoka ofisini mwa Didas na kutoka nje. Huku nyuma akamuacha Didas aliyechanganyikiwa, anaitazama saa yake kila baada ya sekunde kadhaa. Baada ya takribani dakika ishirini simu yake ikaita. Akakurupuka kuipokea baada ya kugundua kuwa mpigaji ni huyu huyu aliyepelekewa mahitaji yake. Didas akapongezwa kwa juhudi zake alizozifanya kukamilisha kile alichoagizwa. "Makubaliano yetu ni kutoziachia video mitandaoni. Kwa hio ziko salama kabisa! Hutozikuta kwenye mtandao wowote ule kiongozi wala usiwe na wasiwasi. Na hakuna mtu awaye yote anayeweza kuzipata." Sauti ya kijana mchangamfu asiyejulikana ikamtoa hofu. "Naweza nikaongeza kiasi zaidi ili zifutwe kabisa kama inawezekana? Samahani lakini." Didas anauliza kwa saut ya nidhamu. "Ninayo furaha kukuambia kuwa hilo haliwezekani mzee wangu!" Sauti changamfu akamjibu. Anayo furaha? Kivipi? "Kwa nini haiwezekani?" Didas akauliza. "Siku yoyote ile utakapolitamka jina la Frola, ama kukutana naye, ama kumuhusisha kwenye mduara wa maisha yako, basi video hizi zitakuwa kama wa muhtasari wa taarifa za habari kwenye televisheni kubwa hapa nchini. Nina uhakika sishindwi kufanya hilo jambo!" Sauti changamfu akaweka kituo kisha akaendelea. "Kiufupi kuanzia muda huu, nataka uachane na Frola moja kwa moja. Huyu nd'o anguko lako! Muone kama ukoma. Kaa mbali naye kabisa. Hapo utakuwa salama." Akamaliza na simj ikakatwa. Didas akachoka. ******* "Kiufupi kuanzia muda huu, nataka uachane na Frola moja kwa moja. Huyu nd'o anguko lako! Muone kama ukoma. Kaa mbali naye kabisa. Hapo utakuwa salama." Yalikuwa ni maneno ya mwisho kutoka kinywani mwa J4 akiwasiliana na mtu kwenye simu. Kando yake ameketi Bebe akiburudika kwa kinywaji chepesi kulipasha tumbo lake kwa ajili ya maandalizi ya mlo mzito uliokuwa ukisubiri hukumu yake pale mezani. J4 akakata simu ile na kumtazama Bebe aliyekuwa anatabasamu kwa madaha. Cheko fupi likawavamia wote kisha wakahamia mezani pale na kuanza kula. "Unawezaje kuyafanya haya yote?" Bebe akamuuliza huku akitafuna paja nono la kuku wa kukaanga. "Ni njaa tu!" J4 akamjibu kwa kifupi. "Njaa? Kivipi." "Njaa amekuwa mwalimu wangu mzuri. Kama hujanielewa endelea kula, ukishiba utanielewa vizuri." J4 akatamka kwa mzaha akiwa na uso unaowaka tabasamu. ------------------- Mambo yamekuwa mambo! Bwana Didas Kilonzo Ambrozi anashambuliwa kutoka kila pande. Ile Utatoa sitoi, utatoa sitoi...Anajikuta anaachia tonge. Anapewa vitisho vikali kutoka kwa mtu asiyemfahamu. Je, huu ni mwisho wa Bebe kukutana na Didas? Ana lengo gani na Bebe huyu J4? Halafu ni kama wana jambo lao hawa...kulikoni? Kazi yetu sisi ni kushare link ya chaneli, kureact na kutoa maoni kwa mwandishi kupitia 0763205351. Riwaya hii tamu Inaendelea...

Post image
πŸ‘ πŸ”₯ ❀‍πŸ”₯ πŸ‘ πŸ™ 7
Image
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
5/31/2025, 11:11:45 PM

*`PAZIA LA FILAMU`* πŸ“½πŸŽ¬ *FREDDY* (2022) Mungu alimbariki sana Freddy Ginwala, Akamuumbia moyo wa dhahabu, moyo wenye utajiri wa adili na ibada. Akamjaalia tabia njema zilizoambatana na adabu iliyotukuka. Mungu akamuongezea na mali za kumtosha alizoridhika nazo hakika. Unadhani Mungu wetu ana kikomo kwenye kumimina neema zake? La hasha! Freddy Ginwala, alikuwa na kazi nzuri ya udaktari wa vinywa na meno. Kazi hii ikampa umaarufu mkubwa kwenye jamii yake. Ikampa heshima na jina bora sana miongoni mwa vinywa vya watu. Freddy angedai nini kingine? Lakini hakika Mungu wetu hatupi vyote! Maadamu sio kila kitu kinatufaa. Na hata kikitufaa, huenda kina muda wake maalumu. Mungu hutupatia vitu hivi kwa muda wake, na muda wake daima ni sahihi! Naam, Freddy Ginwala hakuwa na mwenza wa maisha. Alitamani siku moja akutane na binti mrembo. Amuoneshe namna sahihi ya kulitumikia neno *Nakupenda*. Wapendane kwa damu na nyama, roho na mwili. Wafunge ndoa na wajenge familia bora. Hili kwake lilikuwa ni deni kubwa ambalo nafsi yake ilimdai usiku na mchana. Alikosa furaha na amani. Katika umri wake huu wa miaka takribani 30, hakuwahi kujihusisha na mahusiano katika namna yoyote ile. Sahau kuhusu mazoea na wasichana, Freddy alijawa na aibu kila linapofika suala la wasichana. Akajitahidi kutafuta wachumba wa mtandaoni lakini nao hakuwavutia kutokana na aibu yake na mtindo wake wa maisha. Akaamua kuisubiri bahati yake popote pale ambapo itamdondokea. Ni siku moja tu iliyotosha kumbadilisha Freddy. Naam, siku hii akiwa na bibi yake kwenye sherehe fulani, macho yake yakagota moja kwa moja kwa msichana mrembo wa kike aliyekuwa kwenye hafla ile. Angefanya nini sasa badala ya kumtazama tu? Huu nd'o ujasiri pekee aliokuwa nao dhidi ya wanawake. "Mjukuu wangu, ni lini utakuwa na mke?" Lilikuwa swali kutoka kinywani mwa bibi yake lililogeuka mkuki wa sumu masikioni mwa Freddy. Aibu imemjaa, anatetemeka, hajui amjibu nini bibi yake. Familia yake inamtazama kama mtu wa ajabu. "Haya kuna mrembo yule pale, na anaonekana yuko peke yake. Kamchangamkie upesi, huwezi jua. Nenda usiogope wanawake!" Bibi yake akamsurutisha. Freddy akaenda kuijaribu bahati yake. Huenda ni siku hii bahati imemwangukia, yeye alienda kujaribu tu. Akajikuta ameangukia kwa mke wa mtu. Mrembo Kainaaz! Na ni hapa alipokutana na binti Kainaaz kwa mara ya kwanza. Binti ambaye aliuteka moyo wake, nao ukatii bila shuruti. Akaufunga kwenye gereza la mapenzi. Freddy akawa mtumwa wa mapenzi kwa Kainaaz. Huyu ni msichana pekee aliyempokea na kumsikiliza kwa upole kuliko wale wengine wa mitandaoni. Kwa mara ya kwanza Freddy akajihisi amekamilika. Akabadili mtindo wa nywele zake, akanunua nguo mpya, akabadili mpaka mwondoko! Si amepata mpenzi bhana! Kwa nini asing'ae? Akapenda, akafa, akaoza! Zawadi kemkem hazikukatika kwa Kainaaz. Hakujali kuwa huyu ni mke wa mtu au la. E bwana eee, Freddy amependa tayari. Freedy akiwa anapambana kumfanya Kainaaz aifurahie kila dakika anayoiishi hapa duniani, akagundua kuwa binti huyu anapitia mateso makali. Vipigo na manyanyaso vya kila mara kutoka kwa mume wake vilikuwa kama wimbo wa taifa kwake. Alikuwa amevizoea. Freedy alipoligundua hili, akahaidi kumsaidia. "Niambie ukweli unampenda huyu mumeo?" Akamuuliza kwa moyo uliojaa wivu na kisasi. "Japokuwa ananitesa, bado nampenda. Yeye ni mtu mzuri na mwema sana!" Kainaaz akamtetea. "Namna gani anakupiga kila siku na bado unampenda huyu mtu katili? Haya sikia, ninao mpango hapa...em sogea!" Akamnong'oneza mpango wa siri ambao ungekuwa msaada wa moja kwa moja kwake. Msaada ambao ulipakwa rangi zote za dhambi ya mauti. Mapenzi yale yale yaliyosababisha Ngoswe apoteze nyaraka muhimu kwa ajili ya maendeleo ya nchi, yakamfanya Freddy abadilike na kuwa kiumbe katili. Ama mapenzi yana nguvu sana jama. Akamvizia mume wa Kainaaz usiku usiku katika mida yake ya kufanya mazoezi ya viungo. Akamuua! Akapambana kuuficha na kuufuta ushahidi, akakamilisha uovu wake. Kwake hili lilikuwa ni jambo la kijasiri zaidi kulifanya tangu azaliwe. Alikuwa analipambania penzi lake kwa Kainaaz. Moyo wake ukiwa na ushindi uliosindikizwa na amani na salama, akarejea kwa Kainaaz akiwa na maua mkononi. Hamadi! Hakuamini kile ambacho macho yake yalikishuhudia. Kainaaz alikuwa na mwanaume mwingine. Mwanaume ambaye alitambulishwa kwa jina la mpenzi. Maajabu! Kainaaz alimtumia Freddy kufanya mauaji haya ili tu apate umiliki wa mali za mumewe na awe huru. Shoti ilitambaa kwenye mwili wa Freddy, hakuamini kile alichoambiwa. Akajaribu kumkumbusha Kainaaz ahadi zao na maneno yote matamu walizowahi kupeana. Jambo pekee aliloambulia ni kufukuzwa kama mbwa. Kitendo alichokifanya akikusudia kihesabike kama upendo, kikawa kama pingu za chuma kwake. "Ukiendelea kunifuatilia...nitakushtaki kuwa umemuua mume wangu!" Hakuamini. Ni mapenzi tu. Ni mapenzi ambayo yalimfanya amuuwe mtu asiye kuwa na hatia ili yule ampendaye aishi kwa amani mbali na mateso. Kumbe alikuwa amempenda nyoka mwenye sumu kali. Sumu ambayo inamtambaa kwenye mishipa ya damu yake na kuisuta nafsi yake juu ya dhambi aliyoifanya. Alipenda vibaya, na sasa upendo unampiga visu vya kifua. Freddy Ginwala, Akauzika ule upole na hulka yake ya utulivu. Akavaa kofia mpya ya ukatili. Sasa akawa muwindaji aliye tayari kulipa kisasi katika namna ya kisayansi zaidi. Daktari wa meno akapiga hatua moja kubwa. Simulizi ikageukia upande wa pili. Sasa sio mapenzi tena ni hekaheka na visasi. Ni filamu ya kusisimua yenye mseto mtamu wa hadithi kama asali. Ndani yake kuna mapenzi, visasi na upelelezi wa kisaikolojia. Hutabandua macho yako mara tu utakapoanza kuitazama. Inaitwa FREDDY imetoka mwaka 2022. Imeandikwa na Godlove Kabati ✍🏼

Post image
❀️ πŸ‘ 3
Image
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
6/11/2025, 10:08:25 AM

RIWAYA; *KIBIRITINGOMA* MTUNZI; *GODLOVE KABATI* KWENDA KWA; *MAJIVU YA FASIHI channel* WhatsApp; 0763204351 ----------------- SEHEMU YA KUMI NA TATU *Katu usijidharau na wala usiwadharau wengine.* *Huenda wewe ni daraja la mafanikio ya mtu mwingine, yupo mahala fulani na mtakutana katika namna ya kushangaza.* *Ama neema ya mafanikio yako imebebwa na mtu fulani aliye mbali ama huyuhuyu aliye karibu yako.* *Ulimwengu wetu umeumbwa kwa kanuni ya ajabu sana...* *Tunaishi kwa kutegemeana.* *Karibu kwenye sehemu ya kumi na tatu.* Kila kitu kilikuwa kama mchezo wa sinema. Ndani ya siku moja tu...kila mtu alikuwa amebadilisha historia ya maisha yake. Sio Bebe, sio J4 na pia sahau kuhusu Chief Didas, kama alivyozoea kuitwa na Bebe. Kila mtu kwa nafasi yake, aliyapokea mabadiliko japokuwa katika namna tofauti. Haswaa, Bwana Didas, alilazimishwa kulivujisha pakacha lake. Bebe na J4, wakafurahia nafuu hii ya kuwa wachukuzi. Bwana Didas alikuwa bado haamini kama ameokoka kwenye hatari kama hii. Hatari ya jina lake kupakwa matope mbele ya Watanzania wanaomheshimu. Na zaidi ya yote, wanazipenda bidhaa za kampuni yake. Akashusha pumzi ndefu kujiweka sawa. Ni kama punguani aliyeiokoa kete yake ya mwisho kwenye mchezo wa kamari ambao alikuwa na kila dalili ya kupoteza. Hofu ya kuaibika bado ilizidi kuutafuna ujasiri wake. "Hivi huyu jamaa hajapost kweli?!" Ni swali pekee alilozidi kujiuliza akiwa anaendesha gari lake kuelekea nyumbani. Ameshapiga simu mara kadhaa kwa mkewe, akimuuliza endapo kuna taarifa yoyote ile mpya iliyogonga hodi. "Mh Baba Junior, umekuwaje mme wangu? Hii ni mara ya nne. Mara ya nne unaniuliza kama kuna jipya. Vipi, kwema huko? Ama kuna msiba?" Sauti bembelezi ya kujali, lakini yenye kujiamini ikahitaji majibu. "Aaam...hapana laazizi. Nakujulia tu hali mke wangu. Hehehe wala hamna shida." Didas anamjibu huku akijichekesha kwa aibu. Siku hii anamuita mkewe kwa jina *Laazizi* , haikuzoeleka hivi. Hatulii anabadili upepo angani, atapiga simu kwa baadhi ya vigogo na viongozi wakubwa wa serikali anaofahamiana nao. Hawa atawauliza juu ya kile kinachoendelea Ikulu. Didas atasimamisha gari lake kando kidogo. Anapoongea na watu wenye nyadhifa kama hizi, kelele hazihitajiki. Badala yake ataiinamia simu yake na kulitega sikio lake kwa adabu zote, kusikia litakalosemwa. Hataambulia kitu zaidi ya malalamiko ya viongozi hawa juu ya kero za wananchi na ugumu wa majukumu yao. Ni saa tatu na robo usiku, Didas Kilonzo Ambrozi anarudi nyumbani baada ya siku ndefu sana. Ama siku hii gari la *faza hausi* limerudi nyumbani mapema kuliko siku za nyuma. Tazama, hii ni siku ya tofauti kabisa kwa familia hii tangu asubuhi. Labda ni siku nzuri kwa mama Junior na wanae, lakini kwa Didas ni ya kipekee. Anakuja kupokelewa na bintiye mdogo wa kike katika namna ya *Baba huyo*...anaigiza tabasamu, nalo linamgomea kuigizwa. Anamkwapua na kumuinua juu kiasi lakini hambebi, anamrejesha upya sakafuni baada ya kugundua kuwa amechafuka! Suti yake nyeusi nadhifu aliyoandaliwa na mkewe asubuhi ya siku hii, imepakwa rangi mpya ya vumbi. Tai yenye nembo ya bendera ya taifa, haipo tena shingoni mwake. Ukosi wa shati lake nao ni kama umepata muundo mpya shingoni mwake. Didas anaiburuza miguu yake na kuingia nyumbani mwake akiwa amechoka mwili na akili. Hataki usumbufu wala mazozano na mkewe, ambaye anamshushia mvua ya maswali juu ya muonekano wake. Huyooo Didas anajisogeza bafuni ili akakoge. Lakini hapigi hatua zaidi ya tano kabla hajahisi kuongezeka kwa gramu kadhaa za uzito wa kichwa ni chake. Anayumba na kuisalimia ardhi kwa kuanguka chini kama mzigo. Hii nayo ina maswali ya kumuuliza. Hana majibu...anakoroma tu, anaona giza! Giza linamfumba macho yake. Kinachofuata ni hekaheka za mama Junior na wanae kumpepea kabla hawajaomba msaada wa wafanyakazi wa nyumba ile. ******* "Mic check, mic check...one two, one two!" Sauti nzito changamfu iliendelea kurindima ndani ya Studio kubwa. Ilikuwa sauti ya bwana mmoja mnene wa umbo, aliyeyafunika masikio yake yote mawili kwa kifaa cha kidigitali, maalumu kwa ajili ya kusikiliza muziki, headphones! Fulana yake pana ya kijivu, imelowa jasho na kuchora mfano wa ramani kwenye kifua na mgongo wake. Mbele yake ni meza iliyochafuka kwa vifaa lukuki vya kieletroniki. Vifaa vinavyomweka kwa rangi mchanganyiko. Rangi zinazompa mzuka wa kufanya hiki anachokifanya. Atagusa hapa na pale, atabonyeza kitufe hiki na kile, huku atasugua sugua kisha kile atakizungusha. Ili mradi tu, aukoroge mchanganyiko wa sauti na azalishe mziki bora. Hii nd'o kazi yake.Yeye ni producer (mzalishaji) wa muziki. Pia ni mkufunzi wa wasanii wa muziki wa kizazi kipya. Na siku hii alikuwa akimpika kijana mpya pale pale kwenye studio yake. Kichwa chake kinapanda juu na chini, kikifuatisha miondoko ya mdundo wa muziki anaousikia yeye peke yake. Kisha anatoa ishara ya kidole gumba kwa kijana nyuma ya kinasa sauti, aliye ndani ya chumba maalumu kilichomtenganisha naye kwa kioo kipana kinachoruhusu waonane. Kijana yule anaiweka sawa sauti yake, anayafumba macho yake kiasi kwa hisia kali na kuanza kuimba yale anayoyasoma kwenye karatasi mbele yake, japo kwa kuibiaibia. Hamalizi hata mshororo mmoja wa beti lake, "Hajwaa! Hajwaaa!" Sauti inapazwa, haisikiki. "Dogo achaa! Acha nakwambia! Hii mbovu, mbovu sana!" Bwana yule mnene amechachamaa, anasimama kwa hasira na kufoka. Kitambi chake kinatikisika, ndita zimeweka kambi usoni mwake. "Nimeshakwambia, usiimbie kooni my boy! Sauti itoke kwenye tumbo! Tumboni nimesema! Haya shime..." Anarejea kwenye kiti chake, uso wake mnene bado una ramani za ndita. Ni kama aliyekunywa dawa chungu. Kijana ndani ya chumba, anajiweka sawa kwa mara nyingine. Naye, anavaa kifaa kilekile masikioni. Safari hii anajitahidi kuimba kama alivyoelekezwa. Anaibia mashairi kwenye karatasi mbele yake, kisha anapepesa macho kumsanifu bwana yule mnene, ambaye bado amemkazia macho kwa hasira. Mara ghafla, bwana yule mnene anakitoa kifaa kile masikioni. Anasimama kwa pupa, akimtazama kijana yule. Pumzi zinapishana kwa kasi puani mwake, ni kama mbogo mwenye hasira. "Dogo! Hivi nikueleze mara ngapi? Umekuja kuimba au kunipotezea muda?Mh? Sema!" Akiwa kwenye mahojiano haya na kijana huyu ambaye anaonekana kuipoteza hali yake ya kujiamini. Mara unafunguliwa mlango wa studio hii na kinaingia kikundi cha wanaume watano, kikiongozwa na kijana mmoja aliyevalia mavazi ya kisasa. Nyuma yake ni wenzie wawili wanaoonekana kufanana naye kimavazi, pamoja na watu wawili wa miraba minne, waliovimba kwa mazoezi. Ujio huu unabadilisha hali ya hewa ndani ya studio hii na kusababisha uchangamfu wa ghafla. "Alaaaa! Kenzy kama Kenzy! Finally, you are here my boy!" Bwana mnene anakurupuka na kumkumbatia kijana huyu. "Eeeeh BIG kama BIG!" Kijana yule akamchangamkia. Wanakumbatiana kwa furaha huku kicheko cha ushindi kikikatiza baina yao. "Aiseee...kitambo sana ticha!" Kenzy akatamka kwa bashasha. "Haswaa naona umenitupa mwanangu...mara ya mwisho, lini ilikuwa?...show yako ya pale Mbeya! Tangu hapo!" Bwana mnene, aliyetambulishwa kwa jina la BIG akatamka huku anakielekea kiti chake. "Nimeimiss sana hii studio ticha!" Kenzy anagundua kuwa kuna kijana ndani ya chumba cha mazoezi. "Nani huyu? Chipukizi eeh?" "Yeah...niko namchonga kijana. Sema huyu boga sana aisee...doh!" BIG akatamka huku akilipangusa jasho lake kwa kitambaa kipana. Kenzy akamfanyia ishara kijana yule asogee pale walipokuwa wao. Kijana anasogea akiwa anatetemeka. Haamini kama ni yeye leo hii anaonana na mwanamuziki mashuhuri nchini uso kwa uso. Msanii nyota, ambaye anatamani siku moja aje kuwa kama yeye. "Mambo vipi?!" Kenzy akamuuliza kwa uchangamfu. "Sa..sa-lama bro! Ke- Kenzy. Shkamoo!" Anajiumauma. "N'do nakwambia boy! Mimi nimewaandaa wasanii wakubwa! Huyu hapa Kenzy, nimemchonga mimi. Alikuwa anafuata maelekezo. Anatoa sauti! Kutoka tumboni...haibanii. Wewe sasa!" BIG akatamka kwa kisirani huku akisonya. Wale wapambe waliokuja na Kenzy wakacheka kwa sauti baada ya kuyasikia maneno ya BIG. Kijana akatazama chini kwa aibu. "Unaitwa nani mdogo wangu?" Kenzy amemshika begani kijana huyu, katika namna ya kumfariji. "Jackson" "Hili ni jina lako la kisanii?" "J-la...J-love nd'o jina langu la kisanii" "Safi sana...haya sasa nenda katuoneshe ulichonacho. Jiamini!" Kenzy anampiga begani, kijana anarejea ndani ya chumba. Anavaa kifaa kile masikioni, anashusha pumzi kwa nguvu. BIG anamtazama kwa pembe za macho yake katika namna ya *ole wako na hii uharibu*. Unawashwa muziki na kijana anaanza kutembea na mapigo yake akiimba. Ama! Ni kama mashetani yake yalikuwa yanasubiri ujio wa Kenzy, ndipo yampande kichwani. Sauti yake ikapita kwa adabu kwenye vifaa hivi vya kielektroniki. Ikawa sasa, ni kama mapigo ya muziki ule yanamtii yeye na kuifuata sauti yake badala ya yeye kuyafuata mapigo. Jackson, J-love akamaliza ubeti wake wa mwisho kwa kufumbua macho yake. Akakuta watu wote ndani ya studio hii, vinywa wazi. Makofi! Wote wakampigia makofi! Wote isipokuwa BIG. "Hebuu kwanza!" Bado haamini kama kweli Jackson ameimba namna ile. "Nipe stanza ya mwisho..." Akamsihi huku akicheza na vifaa vyake. J-love akaiimba beti ile kwa ubora zaidi ya mara ya kwanza. Aliyepiga makofi safari hii alikuwa ni BIG peke yake. "Unaishi wapi aisee!" Kenzy akamuuliza akiwa na shauku. "Msasani bro." Akajibu kwa adabu. "Unaimba vizuri sana mdogo wangu. Ukiendelea hivi, nitatoa ngoma moja na wewe siku si nyingi!" Kauli hii ikafufua tabasamu usoni mwa Jackson. "Sauti yako ina kitu mdogo wangu...ina raw energy ambayo wasanii wengi wanaikosa. Usiache, push harder! Na ukiweza kupata mentor kama BIG hapa, usimuachie." Kenzy akaongeza. Wakabadilishana nambari za mawasiliano na kupiga picha ya pamoja. Hili likawa kama kombe la ushindi kwa Jackson. Achana na kupiga picha na staa, hilo si suala. Suala kubwa ni kumiliki namba zake za mawasiliano. "Karibuni aisee wanangu! Sie tupo." BIG akarejea kuutambua ugeni wa Kenzy na wenzie. Ni yeye aliyemtengeneza Kenzy tangu alipokuwa chipukizi mpaka hivi sasa alivyo. Nyota wa muziki wa kizazi kipya. "Naam faza! Nilikuwa nakatiza, nikaona si vyema nipite kwenye mtaa ulionilea halafu nisipite hapa mgodini pasi na kutoa hata salamu!" "Oooh safi sana...walau hata umelikumbuka hilo. Nyie mkitoka huwa mnatusahau. Tumeshawazoea, na wala sishangai!" Producer BIG anajibu kwa kujiamini bado kitambaa chake kipana cha jasho kipo mkononi mwake, kinafanya kazi yake kwa uaminifu. "Walaa mimi siwezi kukusahau anko wangu, BIG mzazi! Tena..." Kenzy anasita kisha mkono wake unazama mfukoni na kuibuka na noti nyekundu kadhaa. "Nadhani hii ya maji itakufaa!" Anampatia BIG kiasi kile. BIG haonekani kushtuka. Anaipokea na kuisweka kwenye mfuko wa suruali lake bila hata kuihesabu. "Mafao yetu ya uzeeni haya!" Anatoa kijembe. Wote wanacheka kidogo. Anamkazia macho Jackson kisha na yeye anazama mfukoni na kumpatia noti ya rangi tofauti na zile alizopewa. "Haya dogo! Changanya mbaliga zako, kaniletee maji makubwa. Chenji inayobaki chukua!" Jackson anaipokea noti ile na kuondoka ndani mule kwa bashasha. "Enhe vipi umefikia wapi na ile project yako mpya? " BIG anamuuliza Kenzy. "Ipi hiyo?" "Video ya lile jiwe lako, ME AND YOU!" Anaweka wazi swali lake. Kenzy anachangamka, "Aaaah ME AND YOU....naelekea kushoot wiki ijayo mzazi. Kila kitu kipo tayari so far! Na pia kuna surprise hapo!" Kenzy anatulia na kuiacha sentensi yake ielee hewani ili auvute usikivu wa BIG. "Surprise gani tena?" "Unajua ni video vixen gani nitakuwa naye?" Akauliza tena kwa bashasha. Lengo lake ni lilelile, amshangaze BIG. "Ni nani?" "Queen Frola!" Akatamka kwa kushtukiza, akitabasamu kwa shauku. Na kweli BIG akashangaa. "Unamaanisha? Huyu huyu mrembo ninayemuona kila siku kwenye matangazo au?" "Eeh huyu huyo. Na mimi nitakuwa msanii wa kwanza kufanya naye kazi hapa nchini!" "Duh hongera bwana. Lakini mbona ni kama ni wa bei ghali sana yule. Utamudu kum-" "Nitamlipa. Pesa sio tatizo. Uzuri ni kwamba nikifanya naye video moja. Itakimbiza sana mitandaoni, faida itakuja kwa kasi!" Kenzy akajipeperusha. "Mh sawa! Utakuwa umepiga hatua kubwa sana aisee. Maana industry haicheki na mtu sasa hivi." BIG akatamka bila kumuangalia Kenzy usoni. "Tena jioni hii nina appoitment naye, tutakutana tuongee." Kenzy akaweka nukta. Baada ya dakika kadhaa za maongezi mafupi hususani ya kisanaa, Kenzy na jopo lake waliondoka na kuacha ahadi nyingine lukuki za kurejea tena. Ahadi ambazo masikioni mwa BIG zilikuwa sawa na baba anayemuhaidi peremende mwanae mdogo ma asimletee. Alishawazoea hawa wasanii! Anawachonga mpaka wanafanikiwa na kupenya kwenye tasnia, wakishapata mafanikio wanamsahau. Ama kweli, Tenda wema nenda zako! Anakunywa mafunda makubwa ya maji na kurejea upya katika darasa lake na kijana Jackson J-love. "Sikiliza, mgema aliwahi kusifiwa sana kuwa anatengeneza pombe aina ya Tembo kwa ustadi wa hali ya juu pengine kupita wagema wote. Unajua ni nini alifanya baadae?" Akamtupia swali Jackson. "Alilitia maji!" Akajibu upesi kwa kujiamini. "Unajibu kwa kuwa umekaririshwa hivyo au unaelewa?" "Naelewa!" Jackson akamjibu. "Haya vaa Headphones tuendelee. Kanuni ni ileile, toa sauti tumboni...imba kwa kujiachia. Usibane sauti! Haya sasa...One! two! three!....twende!" ******* Kipande cha kitu mfano wa kalamu ya rangi kinapitishwa kwa adabu kwenye papi za midomo yake. Anaifumba na kuigusanisha katika namna ya kuikausha rangi ile. Lipstick! Hii ni baada ya uso wake kurembwa kwa vipodozi na kuufanya ung'ae na kumeremeta. Sijaongelea kope zake ndefu ambazo sio za bandia. Ni kope ambazo zikipepesa tu, zinatamfanya mtu anayetazamana naye aimbe pambio kumsifu Mungu. Alikuwa na silaha zote za maangamizi. Kama hatakuua kwa sura yake iliyovimbiwa urembo, basi umbo lake na ngozi yenye nuru havitakuacha salama. Basi tuseme wewe ni mgumu sana. Utapona kwenye haya, lakini chunga sana masikio yako. Labda yafunike kwa pamba usiisikie sauti yake inayoweza kuwatorosha malaika mbinguni. Basi tuseme wewe ni kiziwi japo kwa mkopo. Chunga sana, usimsogelee karibu. Huyu hapa! Anajipulizia manukato yake ya bei mbaya. Manukato yenye harufu tamu, inayodai kumbato zito la mtu atakayepishana naye karibu. Eeh unashangaa?! Inabidi uwe na mkusanyiko wa vilema vitatu mpaka vinne vinavyohusisha milango ya fahamu. Uwe kipofu, macho yako simuone Uwe kiziwi, masikio yako yasimsikie Uwe toinyo, harufu yake ikupite kando. Na katu, ngozi yako isimguse kumhisi...utapagawishwa na wororo wa ile ya kwake. Ulimi hauna mfupa! Hii dhambi sitaki kushiriki. Hamna namna yoyote ile utakayokwepa kukiri kuwa Bebe ni malikia wa uzuri. Hasa jioni hii anayojiandaa kwenda kukutana na Kenzy. Msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini Tanzania. Bongo Fleva! Anasimama mbele ya kioo chake kipana. Anajitazama. Anajigeuza huku na huku, anajibinua kidogo. Kisha anazunguka nyuzi mia tatu sitini kwa madaha. Anafurahi namna nywele zake zinavyoufuatisha mzunguko ule. Ni huu urembo wake uliomtajirisha siku mbili zilizopita. Anatabasamu anapolifikiria hilo. Upesi anaitwaa simu yake, simu janja. Akachukua picha mbili tatu mbele ya kioo kile. Anamtazama yule Bebe mwingine wa ndani ya kioo. Ni kama anaweza kuzungumza naye, anampa uhai, "Enhe una nini sasa? Ulidhani nitakuwa mtumwa daima? Tazama! Mwili wangu unanilipa...tabia ile chafu, uliyokuwa ukinishutumu kwayo, inaeleka kunitajirisha. Upo hapo?!" Anatamka akitazamana na taswira ile. Safari hii huyu Bebe wa kwenye kioo hamjibu na wala habadiliki katika namna yoyote ile. Bali anafanya kile anachokifanya kwa kuigiza. Akicheka naye anacheka, akiruka anaruka. Bebe akatoka ndani ya chumba hiki akiwa na pochi yake ndogo. Anatoka nje akipewa salamu lukuki na vijakazi wake. Anazipokea kishingo upande kana kwamba hazistahili. Na kweli hazistahili! Anajua fika kuwa ima fa ima, muda wowote ule atanyang'anywa mji huu. Anaitazama nyumba hii kwa nje, kisha analigeukia gari lake na kulitazama kwa macho ya aibu. Dhamiri yake inamsuta kwa kutumia kisicho chake. Ilikuwa wazi sasa kuwa ameachana na kampuni ya Bwana Didas. Anaachana na mawazo haya baada ya kukumbuka kuwa hana muda wa kuwaza yaliyopita. Bado kitambo kidogo, atamiliki majumba makubwa hata kumi ya kifahari. Wasiwasi wa nini? Ofa mbalimbali za matangazo bado zimepanga foleni kuhitaji saini yake. Hata jioni hii anaenda kuongelea dili linalohusisha pesa. Ana shida gani sasa? Na zaidi ya yote, amefahamiana na J4. Ambaye ana madili ya maana zaidi yanayohusisha fedha nyingi chekwachekwa. Analiondoa gari lake taratibu na kuanza safari ya kuelekea walikopanga kukutana na msanii Kenzy. "Nipo njiani!" "Ooh okey, mi nimeshafika mama. Nakungoja wewe tu." Ni sauti ya Kenzy ndani ya simu ya Bebe. "Santeeee!" "Take care." Simu inakatwa. Kabla hajaitua chini, inaingia simu nyingine ambayo inaanza kuzungumza papo hapo bila yeye kuiruhusu. "Mlimbwende! Hakikisha anajaa kwenye mfumo huyo msanii. Naona ameshaanza kulainika." Bebe anashtuka. Ni sauti ya J4. "Wewe ina maana umeidukua simu yangu ama?" Anauliza akiwa na hamaniko. "Usiwe na hofu bibiye...mimi nimekutafuta tu kwa muda huu, na kwa bahati nikakuta unaongea na nyama mpya. Nilitaka kukusalimia tu." "Mh kwa nini lakini? Biashara gani hizo unaleta sasa? Masuala ya kudukuana mi staki." "Alaa basi sawa, nitakutafuta usiku." Simu ile ikakatwa. Kukatwa kwa simu hii, kukaambatana na Bebe kupokea ujumbe wa kutoka kwa namba hii ngeni. Ujumbe uliokuwa na ile picha yake nzuri aliyojipiga kwenye kioo chumbani mwake! Maneno chini yameandikwa, *What a beautiful lady!* Imemfikiaje huyu? Hajui. Na wala hata hajaitundika mitandaoni. Bebe akakosa la kufanya, akatabasamu na kuendelea na safari yake. J4 mdukuaji kwenye ubora wake. ---------------- Aisee πŸ₯±, Tukiwa bado tunakitafuta kiini cha riwaya yetu ya *KIBIRITINGOMA*, Fanani wenu ninafurahishwa sana na juhudi zenu za kuisambaza link ya chaneli yetu. Hakika mnastahili kila kilicho bora! Msiache kushare link ya chaneli, acha reaction na toa maoni yako kwenye 0763204351. Mtunzi anapokea yote! Riwaya hii inaendelea...

Post image
❀️ πŸ‘ ❀‍πŸ”₯ πŸ”₯ πŸ«‚ 8
Image
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
6/7/2025, 4:35:42 PM

RIWAYA; *KIBIRITINGOMA* MTUNZI; *GODLOVE KABATI* KWENDA KWA; *MAJIVU YA FASIHI channel* WhatsApp; 0763204351 ----------------- SEHEMU YA KUMI NA MBILI *Kwa kuwa bado tunaishi ndani ya hii dunia..* *Hakika ipo siku moja isiyo jina, utakutana na mtu ama atakuja mtu mpya maishani mwako.* *Huyu ataubadilisha mwelekeo wa maisha yako...atakupa elimu mpya na changamoto ambazo hukuwahi kamwe kukutana nazo.* *Omba sana, mtu huyu mpya asilipeleke motoni jahazi la maisha yako...* *Hii ni sehemu ya kumi na mbili!* Zilipotea takribani dakika thelathini na tano, mpaka walipoukamilisha mlo wao katika hoteli hio kubwa waliokutana. Wakaziteketeza dakika nyingine ishirini kwenye mazungumzo ya hapa na pale huku wakiyasindikiza maongezi haya kwa vinywaji laini. Matumbo na nafsi zao zilipotosheka, ukawadia muda maalumu ambao uliwaweka katika hoteli hii mpaka muda huu. Bebe akaangaza macho yake huku na kule kuhakikisha usalama ambao tayari ulikuwepo. Kisha taratibu bila papara akainama na kuibuka na begi dogo mfano wa briefcase kutoka chini ya meza hii. Sanduku lililoonekana kuwa na uzito baada ya kujazwa vitu fulani fulani, akalitua juu ya meza ile, na meza ikaitika kwa kutoa mlio *TIIII!!* Naam, lilikuwa na uzito usiokuwa wa kawaida. Ni uzito ambao unahitaji dakika moja tu ya maajabu kumbadilisha mtu anayeonekana kama mwehu, aanze kuitwa chifu. Uzito wa fedha! Akalisukuma katika namna ya kuteleza kuelekea kwa J4. J4 ambaye alikuwa na mshawasha wa kuziona hizo milioni mia zilizomo. Akajisogeza karibu zaidi, uso wake ukiwa na shauku. "Mzigo huu hapo, ufungue!" J4 akasita na kumtazama Bebe usoni kwa macho ambayo ni kama yanamuuliza, "Una uhakika kuwa humu ndani kuna milioni mia?" Bila kutamka neno lolote, akayerejesha tena macho yake juu ya sanduku lile. Huenda huu nd'o muda pekee ambao J4 alihitaji kuwa mtulivu. Milango yake yote mitano ya fahamu ikaanza kufanya kazi sawasawa. Akainyoosha mikono yake tayari kwa ajili ya kulifungua. Akili yake ilikuwa tayari imelifungua sanduku hili na kukisia juu ya wingi wa mabunda makubwa ya fedha uliomo ndani yake. Na sasa alikuwa akienda kuyahakiki yale aliyokuwa akiyadhahania akilini mwake mubashara kabisa. Milioni mia! Alaaa, hii ilikuwa fedha ambayo hakika asingewahi kuimiliki mpaka atakapozama futi sita ardhini. Mikono inamtetemeka, J4 akavibetua vyuma vilivyolikaza sanduku lile. Kisha kama anayefungua mlango hivi, akalifungua sanduku. Hamadi! Pua zake zikapokelewa na harufu ya kipekee. Harufu halisi ya fedha kutoka sandukuni. Mboni za macho yake zikapanuka, macho yake yakaona, Safu za mabunda ya noti mpya nyekundu zilizonyooka zilijipanga vyema kama zimepigwa pasi. Bado haamini, mkono wake hakukutaka kubaki nyuma. Akaamua kuzigusa. Mkono wake ukatambaa na kuteleza juu ya noti hizi. Vidole vikakana kuwa havijawahi katu kuzigusa milioni mia moja. Akafanya kama anayechimba, akaibuka na bunda moja la noti zilizoviringwa ndani ya mpira mdogo. Akalitikisatikisa kama anayepima uzito wake. Akazichezesha noti kwenye ncha za vidole vyake kama anayezihesabu hivi. Ni noti mpya kabisa ambazo hazijapita kwenye mikono ya watu wengi. Uso wake ukawa wa mwisho kudhibitisha kuwa amefurahishwa sana na kile alichokikamilisha. Tabasamu likawaka usoni mwake, akamtazama Bebe usoni. Akaufungua mpira ule uliozidhibiti noti za bunda lile, zikawa huru. Akazitupa juu ya meza kumwelekea Bebe. Noti zikateleza mezani katika mfumo wa kusambaa. "Unajua tunaziitaje hizo?" J4 akauliza akiwa wima. "Zinaitwa hela!" Bene akamjibu kwa bashasha. "Lipe neno uzito...sema fedha! Kama wasemavyo wao." J4 akarejea kwenye kiti. Akauinua mguu wake wa kulia na kuubebanisha juu ya paja la ule wa kushoto, akakaa kwa kuchonga namba nne. "Ni burudani sana kutazamana na utajiri uso kwa uso. Na leo nimepata bahati ya kuipata burudani hii bure kabisa. Kwa nini nisiburudike?" J4 akatamka huku akilifunga upya briefcase lile. Bebe akacheka kidogo huku akiuziba mdomo wake kwa aibu. "Haya nd'o maisha tunayotakiwa kuyaishi Bebe!" J4 amemaliza kulifunga sanduku lile na sasa anafanya jitihada ya kuzikusanya fedha zile alizozitawanya mezani pale kwa mbwembwe. "Hii ndio namna tutakavyo-yanyanyasa maisha. Mpaka yapige magoti yakisota na kuomboleza chini ya nyayo zetu. Hivi hivi...mimi na wewe!" Sauti yake imejaa unabii, J4 anatamka akiwa ametazamana na Bebe uso kwa uso. Wote wakatabasamu wakitazamana. Tabasamu lao lilinena lugha moja. Lugha ambayo waliielewa wao tu. Sio lugha ya mapenzi asilani. Ilikuwa lugha ya ajabu ambayo Bebe aliitafuta kwa muda mrefu sana bila mafanikio. Lugha ya ukombozi! Ni lugha hii hii iliomfanya akutane na J4 na kumkabidhi uaminifu wake wote. Hakuwahi kumuamini mwanaume yeyote yule lakini kwa J4 ilikuwa tofauti. "Tutakuwa huru...tutakuwa matajiri! Ni haya haya maisha yaliyotufikisha hapa tulipo. Mimi na wewe tunajua ni nini tunakihitaji." Ni maneno ya J4 yaliyogeuka kuwa asali masikioni mwa Bebe. Maneno ambayo baadae yalimfikisha Bebe kwenye anga ambazo hakuwahi kutarajia kufika. Anga zinazoifanya simulizi hii iwe hii. ******* Ilikuwaje mpaka wawili hawa wakakutana? Ni swali ambalo hakika linakufanya unishutumu mimi ninayekusimulia. Ilikuwa hivi... Jumanne Maliki, ama J4 kama mlivomzoea ndiye alikuwa mchoraji wa hii ramani yote. Mpango wake aliusuka kwa ustadi na hakutaka kupoteza muda kabisa. Hapo awali, Akiwa katika harakati za ujana maji ya baridi na swahibu yake Dotto, alipagawa alipoitia sura ya Bebe kwa mara ya kwanza kwenye mboni za macho yake. "Hii pisi kwelikweli aisee, imenyooka sana hii!" Dotto aliinadi picha ile kwenyw simu yake. "Anaishi wapi huyu? Mbona sijawahi kumuona hapa mtaani." J4 akahoji. "Aaa wewe...unadhani hiki kiwango ni cha kucheza kwenye viwanja vya chandimu? Hiki ni kiwango cha kimataifa kaka. Class A kabisa! Wa watu wazito hawa!" D akaanza mbwembwe zake zilezile za udalali. J4 akampokonya simu yake na kuitazama picha ile kwa umakini zaidi. Akakitikisa kichwa chake kukubaliana na alichokiona. "Mali iko Sinza hii mzee baba. Inapiga ukaunta pale GRANDE!" Dotto akaendelea kuipamba picha yake. "Ni baamedi eh?" "Itakuwa...lakini ninasikia, japo sina uhakika...kuwa ni dada poa!" D akanong'ona. Hili la mrembo huyu kuitwa dada poa, likazitia doa kubwa jeusi sifa zote nyeupe zilizokuwa zikipepea kwenye akili ya J4. "Kwamba anajiuza au?" "Nasikia hivyo...maana yule bimdashi mmiliki wa klabu, nasikia nd'o mishe zake hizi pande zile." "Duh anaitwa nani aisee?!" "Nani? Huyo bimkubwa au-" "Huyu demu" "Be-Bebe! Anaitwa Bebe!" Anaitwa Bebe! Nd'o ikawa sentensi ya kwanza kukisumbua kichwa chake. Akamhimiza rafiki yake himahima ampeleke pale kwenye klabu ambayo mrembo huyu anafanya kazi. Siku ya kwanza, wakafukuzwa na walinzi baada ya mavazi yao kuwatambulisha kama vijana mabarobaro waliokuja kutalii na kuondoka tu. Hawakujipanga, bali walikurupuka tu. LE CLUB GRANDE sio mahala pa wanaoulizia bei. Wakajipanga vyema siku ya pili, lakini haikuwa bahati yao. Hawakumkuta! Baada ya J4 kubembeleza sanaa, Wakajaribu tena siku nyingine. Safari hii wakaenda usiku. Na kweli, akamuona Bebe kwa mara ya kwanza. Moyo wake ukamuuma sana! Ni heri asingemuona kabisa labda angeweza kujiepusha na yote. Kwamba hii sanaa bora ya uumbaji inayopumua ni kahaba? Alikataa kuamini. Moyo wake ukataka kufanya kosa la kumfumba macho na kumtupa kwenye shimo la huba. Lakini akili yake ikawahi upesi na kuikamata miguu yake, ikamrudisha kwenye njia sahihi. Kwamba azame penzini na kahaba? Akili yake ikamshutumu na kumfanya ajidharau. Lakini moyo uliougua gonjwa la mapenzi unatibika kwa namna ya kipekee sana. Na tiba yake ya kweli ni muda! Naam, kama ambavyo alimpenda taratibu. Ni hivyo hivyo alijifunza kumsahau taratibu. Na katika darasa hilo la kujifunza kumsahau, akadurusu somo ambalo alitaka limpe sababu zenye mashiko, ni kwa nini asimpende kahaba. Hapa akaiacha nadharia, akajifunza kwa vitendo. Akaanza kumfuatilia Bebe nyendo zake zote alizotegemea ziwe chafu machoni mwake. Yeye alikuwa na lengo moja tu. Kujifunza kumsahau. Hilo tu. Lakini macho yake kijana huyu mhitimu wa uhandisi wa umeme na masomo ya kompyuta, yakaiona fursa! Fursa ambayo labda aliwahi kuiona na kuipuuza. Lakini sasa anapata kila sababu ya ni kwa nini anahitaji sana fursa hii. Akazidi kuzama darasani! Aliyaona macho ya wanaume wenye tamaa, yanavyolitazama umbo la Bebe na kummezea mate. Aliyaona macho yao yanavyoweweseka baada ya kutazamana na ile sura yake jamali. Tazama wanaume hawa wanavyomwaga fulusi za kutosha ili tu wampate Bebe kwa ajili ya kuiridhisha miili yao. Tazama namna wanavyoteketeza fedha ambazo labda zingetosha kabisa kubadilisha maisha ya J4 na wazazi wake kule Ushirombo. Wanaume hawa ndimi zao zinaning'inia nje wakitokwa na mate kwa uchu wa ngono. Macho yao yanawaka tamaa wakimtazama Bebe. Tazama! J4 akafumba macho yake na kuzikumbuka nyakati na maisha yote magumu, yaliyogubikwa na umasikini aliyoyapitia tangu akiwa chuoni hasa baada ya kukosa mkopo wa serikali. Akalazimika kukitumia kipaji chake akidukua vyanzo mbalimbali vya mitandao na kuuza intaneti kwa wanafunzi wenzake ambao nao walimlipa kwa rasharasha. Mara kadhaa akakoswakoswa kudakwa na vyombo vya usalama kama mhaini na tapeli wa mitandao. Yote haya aliyafanya ili tu apate fedha ya kujikimu. Leo hii yupo mtaani, anatumia kipaji chake kama silaha ya kuiwinda fedha. Lakini hapa anaona fedha ile inamwagwa na matajiri kwenye uasherati. Ajabu! Vita yake ya kuitafuta fedha ikamdai silaha ya ziada. Hapa akamtazama Bebe kama silaha yake mpya ya maangamizi. Alikuwa amemfatilia kwa muda mrefu. Mpaka Bebe anapata umaarufu, J4 alikuwa kimya nyuma ya skrini za kompyuta akiandaa mitego yake ambayo aliiamini sana. Na alihitaji nyakati moja pekee ya kuitega mitego hii. Ndipo ikafika hii siku ambayo aliwafuata Bebe na Didas hotelini kwa usiri. Akalazimisha kumpiga Bebe kikumbo mpaka vitu vyake vilivyokuwa ndani ya mkoba legevu vikaanguka chini. Katika kumsaidia kuviokota, mikono yake ikafanya kazi kwa kasi ya ajabu na kubandika vinasa sauti na kamera ndogo ndogo kwenye baadhi ya vitu vyake. Akiwa na uhakika kuwa ni lazima tu atanasa. Na kweli akanasa! Ilikuwa bahati mbaya sana kwa bwana Didas Kilonzo Ambrozi. Ndani ya muda mchache, tayari J4 alikuwa na vipande vya video kadhaa ambavyo aliviunganisha. Usiku wa siku ile akakutana na Bebe baada ya kumpigia na kumueleza kuwa upo ujumbe wa siri anaotaka kuzungumza na yeye peke yake. Akamuondoa hofu kuwa kwa usalama zaidi, Bebe yeye mwenyewe apange mahala ambapo angependa wakutane. Bebe alipojaribu kuleta maringo, akashtuliwa kwa kipande cha video ile kilichotumwa katika simu yake. Hapo akakurupuka na kukutana na J4. Saa nne usiku, LE CLUB GRANDE! Ni hapa ambapo Bebe alipaona kuwa mahala salama zaidi kutokana na kujulikana kwake mahala pale. Hapo akakutana na J4 kwa mara ya kwanza, wakazungumza. "Wewe ni nani? Hiyo video umeitoa wapi?" Bebe aliuliza akiwa mwingi wa hofu. Licha ya uzoefu wake wa kuwahudumia wanaume kingono, hakuwahi katu kujirekodi au kuruhusu hilo litokee akiwa kazini. "Jina langu utalifahamu mara tu baada ya mimi kukamilisha kile nilichokusudia kukifanya ili wote tufaidike. Namaanisha, nikusaidie wewe na wewe unisaidie mimi." J4 akiwa ndani ya kofia pana na mavazi yaliyojaribu kumfanya aonekane kama jasusi wa kimataifa, akatamka kwa kujiamini. "Unisaidie? Nikusaidie?...wewe unanisaidiaje mimi? Unaweza kunisaidia kwa lipi?" Bebe akaruhusu kiburi kimfanye ajihisi yeye ni jitu la miraba minne na huyu anayeongea naye ni mbilikimo tu. J4 akatabasamu kidogo kisha akaketi vyema. "Sikia Frola!" Kutajwa kwa jina hili kukamfanya Bebe aubadili mkao wake na kukaa chonjo. "Mimi nafahamu fika wewe ni mwanamke wa aina gani. Nafahamu fika kuwa unapenda kuwa huru, ulitoka hapa GRANDE ili uwe huru. Hata huko ulikoenda, unautafuta uhuru! Lakini bado maisha yako, yako ndani ya minyororo ya utumwa. Haujapata kile unachokitafuta." Akatulia na kuyapa nafasi maneno yale yazame kwa Bebe. "Uhuru? Unadhani mi ni mtumwa?" Jazba inaanza kumpanda Bebe. "Hii video hii...inaweza kukupa fedha mara ishirini ya huo mshahara wako wa milioni mbili na nusu unaopata kwa ajili ya tangazo moja unaloigiza! Huwezi kuamini." J4 akatema cheche huku akitikisatikisa simu yake ya kupangusa, iliopasuka kioo chake na kuacha nyufa kadhaa zikitambaa. Bebe akapagawa. Huyu jamaa anajua mpaka mshahara wake! "We..ume..umejuaje mshahara wangu?" Akababaika. "Nataka nifanye kazi na wewe Frola! Kazi yetu tukiwa huru, mimi na wewe. Nakuhaidi tutapata hela nyingi sana! Tutakuwa matajiri." Utajiri? Utajiri gani hasa ambao Bebe alikuwa akihuitaji kutoka kwa huyu kijana mpya machoni mwake? Tayari anao umaarufu mkubwa nchini japokuwa huu haukumfanya awe tajiri moja kwa moja. Hata kama angepata ofa yenye malipo makubwa, bado isingeweza kuzidishwa mara ishirini ya mshahara wake. Akaketi vizuri na kuiegemea meza yake, akajisogeza karibu, tayari kumsikiliza J4. J4 akaachiwa umiliki wa dimba la maongezi. Akauweka mezani mchoro wake mzima wa namna atakavyoikamilisha mipango yake yeye na Bebe. Maneno yake yakawa sumu kali ambayo iliulegeza moyo wa Bebe, supastaa. Bebe akalainika na kukubaliana moja kwa moja na mpango ule wa J4. Mpango ambao ulimhakikishia kuwa siku inayofuata, atakuwa na zaidi ya milioni hamsini kibindoni. Ulikuwa mchezo rahisi sana kwake...ugumu wote uliachwa kwa J4. Ni ndani ya siku mbili tu. Muda huu wanatazamana na kisanduku kilichosheheni fedha. Milioni mia! "Huu ni mwanzo tu! Bado kuna mtu fulani huko ametutunzia hela zetu. Inatakiwa anase kwenye mtego wetu upesi." J4 anayasema haya baada ya mgawo kufanyika kama walivyokubaliana. Na sasa kila mmoja amekifutika kiasi chake anapopafahamu. Wako ndani ya gari la Bebe alilopewa na kampuni ya Bwana Didas. Muda mchache tu ujao, anafahamu kuwa ataachana nalo. "Kituo kinachofuata?" Bebe akamuuliza mikono yake ikiwa kwenye usukani. "Hakuna oda yoyote ile ya mtu binafsi ambayo umeipokea?" J4 akamuuliza. "Ooh yupo, Yule msanii Kenzy. Aliniomba niwe naye kwenye rekodi ya moja kati ya nyimbo zake za hivi karibuni." Bebe akachangamka. "Basi nadhani unajua ni nini unatakiwa kufanya." J4 akanong'ona kisha akatoa cheko la kibabe. Cheko la fedha! Akafungua mlango wa gari hili na kuanza kutoka nje. "Wapi sasa, si ninakupeleka mpaka kwako au?" "Hapana, ukifika wakati wa wewe kupajua kwangu. Nitakuleta mwenyewe. Mahusiano yetu hapa ni ya kibiashara tu na si vinginevyo..." J4 akatamka kwa kujiamini tayari yuko nje ya gari. "Mawasiliano yako ni yalayale ama?" Bebe akapaza sauti. "Hapana hayo yameshapotea, hayapo tena hewani....nitakutafuta kwa namba mpya." J4 akamjibu akitokomea. Hakumng'ang'ania Bebe kwa lolote na wala hakuonesha kumjali. Hili ndilo lililomuacha Bebe njia panda. "Ni mwanaume wa aina gani huyu?" Akajiuliza. Amekutana naye jana usiku tu...lakini tayari amemzoea kama ndugu mapacha wa tumbo moja. Na hajaweza kubabaishwa na urembo wake. Bebe akaliondoa gari lake eneo lile huku akilitafakari ombi la kijana huyu mwenye uelekeo wa hirimu moja na yeye. *Alitaka wawe na mahusiano ya kibiashara!* hivyo tu. Akazikagua noti zile mpya ndani ya mkoba wake, akazikuta bado zinapumua. Akatabasamu. Ama hakika, alikuwa kwenye biashara. ------------------------ Milioni mia kutoka kwenye vibubu vya bwana Didas, imepasuliwa na kutulizwa kwenye mifuko ya Jeifoo na Bebe. Pacha ambayo imetuhaidi kuhusiana kibiashara katika namna ya kushangaza. Wamemtaja Kenzy, msanii wa kizazi kipya ambaye ni maarufu pia nchini. Ni bomu gani limeandaliwa na pacha hii matata? Share link ya chaneli, acha reaction na toa maoni yako kwenye 0763204351. Mtunzi anapokea yote! Riwaya hii inaendelea...

Post image
❀️ πŸ‘ ❀‍πŸ”₯ πŸ”₯ 13
Image
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
5/22/2025, 8:43:44 PM

RIWAYA; *KIBIRITINGOMA* MTUNZI; *GODLOVE KABATI* KWENDA KWA; *MAJIVU YA FASIHI channel* WhatsApp; 0763204351 ----------------- SEHEMU YA TISA *Usijidaganye...* *Siri ni ya mtu mmoja tu.* *Ikiwa ya wawili hiyo siyo siri tena, itatambaa kwa kasi ya ajabu...ikiwa na onyo lilelile la "Usimwambie mtu, hata mimi nimeambiwa nisiseme."* *Hii ni sehemu ya tisa.* TAHARUKI! Aliyafikicha macho yake kwa viganja vya mikono yake ili ajihakikishie kuwa ile sio ndoto. Kisha akaigeuza ile simu ili aone kama ni ya kwake au labda ni ya mtu mwingine. Nayo ikawa ni kama inamwonya kuwa chondechonde, asiikane. Akaitambua kuwa ni simu yake. Hayo hayakutosha. Akaitazama video ile kwa mara nyingine. Mara ya nne. Akajihakikishia kuwa hawa viumbe wanaopinduana kwenye video hii anawatambua. Huyu wa kiume hakumtambua kwa sura na majina tu, alimtambua mpaka kiroho na kimwili. Alikuwa ni yeye mwenyewe. Didas akajipapasa mfukoni mwake na kutoa leso. Huku akiitazama simu yake, akajipangusa matone ya jasho yaliyokuwa yameanza kuota kimafungu kwenye paji la uso wake. Yakatengeneza michirizi kwenye shingo lake. Simu ikamponyoka na kuanguka sakafuni. Hapa akagundua kuwa hata mwili wake ulimtetemeka sana, ni kama ulioshtushwa na video hii ya ajabu. Akainama na kuikota upesi akichelea kuonekana na mtu yeyote eneo lile licha ya kwamba alikuwa peke yake eneo hili. Asubuhi hii ya saa tatu kasoro, joto la mwili likamzidia. Koti la suti yake nadhifu akaliona kama mzigo mkubwa wa kilo hamsini juu ya mwili wake, akalivua. Tai yake shingoni akaiona kama kitanzi kilicho tayari kumpa mkataba wa kuiaga dunia, akailegeza katika namna ya haraka mpaka akaichomoa katika fundo lake. Didas alibabaika. Eneo lile ambalo dakika kadhaa nyuma aliliamini kama eneo lake bora kwa ajili ya mapumziko, akaliona sio salama tena. Simu yake akaiona kama bomu ambalo muda wowote linaweza kulipuka kama tu ikiwa mkononi mwa watu wengine. Akaitia kwenye mfuko wa suruali lake kwa umakini mkubwa kisha akapiga hatua kubwa kubwa kukitafuta chumba cha ofisi yake. Njia nzima kuelekea ofisini mwake, macho yake ni kama yametiwa kiwi. Hakuona wala kutambua mtu au kitu chochote. Wafanyakazi wakamshangaa, "Bosi amekuwaje tena?" Waliulizana na hakuna aliyekuwa na majibu. Siku hii Didas alionekana kuwa wa tofauti kwao kuanzia asubuhi. Aliwahi mapema kabla yao, alikuwa mwenye tabasamu na bashasha tele usoni na alikuwa mchangamfu mno kuliko walivyomzoea. Lakini ajabu ndani ya kipimo cha masaa mawili kama sio moja, Bosi wao Didas huyu hapa amebadilika. Miguu yake inapishana kwa kasi koridoni. Anahema juu juu, koti mkononi, tai imemlegea shingoni. Didas amepagawa! "Sipokei simu wala mtu yeyote kuanzia muda huu. Nina kazi ya maana sana naifanya ofisini, sitaki usumbufu!" Yalikuwa ni maagizo yaliyotolewa na sauti inayoamrisha kutoka kwa Didas kwenda kwa karani wake. "Sawa bo-" Hakusubiri jibu. Upesi akauvamia mlango wa ofisi yake na kuzama ndani, kisha akaubamiza mlango kwa nguvu na kitasa kikasikika kikitekenywa na ufunguo kwa ndani. "Kha! Kulikoni tena?" Karani huyu mrembo wa kike ,akapigwa na butwaa. Huko ndani, Didas akazima kila kifaa cha umeme alichokiona kwa hofu ya kuvujisha kile anachotaka kukifanya, safari hii hakutaka kufanya makosa. Akaikagua ofisi yake kwa umakini akihofia kuwa labda kuna vinasa sauti vilivyotegwa, visije vikamtia upya majaribuni. Aliogopa sana. Akamuogopa sana yule mtu aliyempigia simu na kumpa maelekezo kama haya yaliyoambatana na hii video ya aibu. "Ameturekodi muda gani huyu hayawani?" Akajiuliza yeye na nafsi yake. Kabla hajaanza kugawanya lawama, akajipa dakika chache za kukaa na kutafakari. Akiwa ameketi juu ya kiti chake kikubwa kinachonesa qmbacho muda huu kilikiwa kigumu kama chuma, akavua shati na kubaki na fulana. "Labda pale hotelini walitufanyia uhuni? Au...walitega kamera kwenye koti langu? Au Bebe...hebu ngoja!" Akaipekua orodha ya namba za mawasiliano kwenye simu yake, akitafuta namba ya Bebe. Akampigia, simu yake haikupokelewa. Akampigia mara ya pili, ya tatu na ya nne bila mafanikio. "Shit!" Akasonya na kupiga ngumi juu ya meza yake kwa nguvu. Akiwa kwenye taharuki, akajikuna kidevu chake kilichosheni ndevu nyingi. Fikra zake zikapaa na kumuonesha kila rangi ya hatari ambayo hakuwahi kuomba imkute maishani mwake. *"Hiki ni kipande kidogo tu cha keki nzima."* akausoma upya ule ujumbe ulioambatana na video ile. Safari hii aliuona ni kama umeandikwa kwa mwandiko wa kishetani, na aliyeuandika anamcheka kwa dharau. Didaa akatetemeka kwa hofu. "Ni kipande cha keki. Labda ipo au zipo ndefu zaidi ya hapa. Labda huyu jamaa video zangu za siku nyingi, hata kabla ya hii ya jana." Akatamka kwa huzuni. "Vipi...vipi kama akizitundika video zote mitandaoni na watu wa rika zote wazione. Nitaweka wapi sura yangu mimi Dida?!" Akahamishia mikono yake kichwani. Kumbukumbu zake zikamsulubu, zikimkumbusha matukio na matendo yake yote maovu aliyoyafanya na Bebe. Chozi likamdondoka! Akafikiria namna atakavyoaibika, namna atakavyoichafua sura ya kampuni. Akaona waziwazi atakavyoporomosha soko la bidhaa zao, atakavyouangusha ufalme wa biashara uliojengwa kwa muda mrefu tena kwa jasho, machozi na damu. "Eeh Mungu wangu!" Macho yake yakawa ya moto kwa machozi. Alikuwa na muda mrefu tangu ametoa machozi, lakini leo hii hofu ya matokeo ya kumbukumbu ya dhambi zake za nyuma, inamtoa machozi. Alipokumbuka kuwa hata mwanaye mkubwa Junior ana simu janja aliyompatia kama zawadi, Didas Ambrozi akahama kutoka kwenye kiti na kuchutama sakafuni. "Shenzi kabisa!" Akafoka kimyakimya. "Mtoto mdogo kama yule anamiliki vipi simu ya mkononi?" Haikujulikana kama anamlaumu mwanaye aua anajilaumu yeye mwenyewe aliyempatia. Mwanaye ambaye nd'o kwanza yuko elimu ya msingi, darasa la sita. Tena ni mjuvi na mtundu wa kuperuzi kwenye mitandao ya kijamii. Hakuna kurasa yoyote ya watu maarufu ambayo hakuijua. Didas siku zote alichekelea na kudai kuwa hiki ni kizazi kipya, kizazi cha teknolojia, hivyo haoni kosa la mtoto mdogo kuijua mitandao na kuitumia. Alichoka! Fikra hii ikaambatana moja kwa moja na matokeo baada ya mkewe kuiona video hii ambayo aliitafsiri kuwa ni video chafu. Kwa nini hakukifikiria kitendo kile alichokifanya kuwa kichafu na badala yake aichafue video? Alijua mwenyewe. Kwa mara nyingine akaona kuwa huenda hii ikawa hoja kubwa na yenye mashiko kwa mkewe anayelumbana naye kila uchwao. Akaifikiria heshima aliyojijengea katika kanisa lake la kiinjili analoabudia, heshima na busara zake vikampatia cheo cha kuitwa *mzee wa kanisa*. Hamadi! "Nitapoteza kila kitu!" Akatamka kwa sauti ya chini huku akipambana kulifuta jasho usoni mwake. "Kwamba magazeti yataaandika, SAKATA LA MREMBO FROLA NA BOSI WAKE LAITETEMESHA DAR." Akawaza. Hakutaka kusubiri mashambulizi haya ya kushtukiza yamfuate alipo... Akaamua kujihami kwa silaha alizo nazo. Na silaha yake kubwa aliyoitegemea muda huu ni pesa. "Anataka fedha huyu. Aseme kiasi chochotekile anachokitaka nitampatia! Ili mradi tu, aniondolee hii aibu!" Akaamua aipigie namba ya mtu yule asiyemfahamu. Ikapokelewa upesi. Akaanza kujitetea mara moja, "Nakusikiliza wewe. Niambie unataka nikulipe sh'ngapi? Nitajie kiasi unachokitaka tuyamalize." Akatamka kwa jazba iliyochanganyikana na woga. "Kunilipa? Kiasi? Sielewi unaongelea nini mzee wangu." Katika namna isiyotegemewa sauti ile ikajibu kwa utulivu. "Come on! Nisikilize kijana...usitake kushupaza shingo yako bwana. Ni matarajio yangu kuwa unaelewa ni nini namaanisha. Tafadhali, niambie unataka kiasi gani tuimalize hii kesi." Didas akirejea taratibu juu ya kiti chake akarusha karata yake nyingine. "Mzee...mimi nimebahatika kukufahamu japo kwa jina, lakini wewe hunijui. Nimefanya wema wa kukutumia kipande cha keki tufaidi pamoja. Na nikakueleza kuwa uniafute ili tujadiliane juu ya ladha yake, hivyo tu!" Akamalizia sentensi yake akiwa na cheko la dharau. Didas akazidi kuchanganyikiwa, akatoka kwenye kiti chake kwa mara nyingine, akaanza kutembea akizunguka zunguka mule ndani. Alitamani amjibu kwa kumrushia matusi mazito lakini wakati huu alihitajika awe mjinga na mnyonge, akachagua kubaki kimya. "Nisikilize mzee wangu..." sauti ile ikatangaza ubabe. "Maelekezo yote atakupatia huyo malaya wako. Ni maelekezo yanayohitaji utekelezaji wa haraka, mna siku moja tu. Ama sivyo vyombo vya habari na mitandao vitapata habari mpya inayovutia!" Sauti ile ya kukoroma ikaweka kituo na simu ikakatwa! Moyo wa Didas ukaruka mapigo kadhaa baada ya kusikia maneno yale. Kwa mara ya kwanza maishani mwake akamuweka Bebe katika orodha ya viumbe hatarishi wa kuogopwa. Akawa na asilimia zilizotosha kuvunja imani yake kwake. "Kumbe anahusika!" Donge kubwa la hasira likajiunda kifuani mwake. Akiwa harakati za kuvaa upya mavazi yake ili aondoke ofisini mule, simu yake ikaita. Mpigaji sio mwingine bali ni Bebe. Akashusha pumzi na kuitazama simu ile. Akaipokea akiwa anatukana matusi mengi kimoyomoyo. Lakini ajabu! Akapokelewa na sauti ya kilio na malalamiko. "Daddy...tuna siku moja tu Daddy!" Bee alikuwa analia na kuomboleza. Achana na kilio chake wala maombolezo yake. Kilichomzuzua Didas ni ile sauti nzuri na tamu ya Bebe, hasa akiwa kwenye kilio. Hata kama angekuwa anaigiza, kilio chake kingetosha kabisa kumpa msamaha na akauepuka moto wa milele. "Kuna nini Bebe? Mbo..mbona unalia eh?" Didas anazuga haelewi kinachoendelea, amevaa ujasiri bandia wa kiume. "Ametupa siku moja tu mpenzi wangu...siku moja tu!" Kitendo cha kuitwa *mpenzi* kikawa kama msumari wa moto kwenye kifua cha ujasiri wa Didas. Akasahau hasira yake yote aliyokuwa nayo dhidi ya Bebe. Akachukua jukumu la kumbembeleza na kumuondoloea hofu. "Usijali kipenzi...kila kitu kitakuwa sawa. Hili nitalimaliza mimi mwenyewe dear. Huyu nyang'au nitamtia adabu, hatatuchezea michezo yake tena! Uko wapi sasa hivi?" Didas akajitutumua na kuonyesha uanaume wake. Bebe akamueleza kuwa yuko nyumbani kwake. Wakapanga mahali pa kukutana ili wachore ramani ya kuokoa kwenye msitu huu mpya walioingia na kupotea ndani yake. Didas akiwa na huruma tani mia kwa Bebe. "Huyu dogo atanitambua mimi ni nani!" Akaweka nia yakumuangamiza huyo aliyewachezea mchezo huu. Hakujua! Hakujua! --------------------------- Itaendelea Jumamosi Tuendelee kusambaza link ya chaneli na kutoa maoni yetu kupitia 0763205351.

❀️ ❀‍πŸ”₯ 4
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
6/9/2025, 7:02:29 PM

Jama mnamkumbuka Ferouz?... Eeh yule Ferouz Adam kinyozi... Aliyeenda kutafuta pesa, akakutana na mabazazi... Kutoka hapo...tukapata riwaya bora ya hiki kizazi... 🀭 E bwana eeh! Riwaya ya *SHAMBA LA HELA* itakamilika Ijumaa hii. Itakuwa kwenye mfumo wa nakala laini yaani PDF. Ni riwaya ya hekaheka, mapigano na mavarangati... Ni msitu wa maneno zaidi ya *Elfu hamsini na moja* kwenye kurasa zaidi ya 350. Ni kalamu ya yuleyule fanani wenu Godlove Kabati. Kwa nini uikose kazi hii adhimu?

Post image
❀️ πŸ‘ ❀‍πŸ”₯ πŸ‘Š πŸ”₯ πŸ™ 13
Image
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
5/26/2025, 7:49:44 PM

RIWAYA; *KIBIRITINGOMA* MTUNZI; *GODLOVE KABATI* KWENDA KWA; *MAJIVU YA FASIHI channel* WhatsApp; 0763204351 ----------------- SEHEMU YA KUMI *KUMBUKA...* *Usimpe mwanadamu asilimia zako zote za uaminifu, hasa kila linapofikia suala la pesa.* *Hapa usishangae sana yule rafiki yako unayemuamini atakapogeuka na kuwa kama mnyamamwitu mkali, aliyetayari kukurarua!* *Mungu alimuumba mwanadamu,* *Mwanadamu akaiumba fedha,* *Ajabu! Fedha iliyoumbwa na mwanadamu, inamchanganya na kumuweusha.* *Tafsiri kadri ya uelewa wako!* *Na hii ni sehemu ya kumi...* Lilikuwa ni anga la saa saba mchana, lililomiliki jua la utosi, jua linalofukuta joto zito linalokera lakini lililozoeleka haswa kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam. Jua hili liliendelea kufanya ukatili wake kwa watu wenye vichwa vyenye mtindo wa nywele aina ya *kipara* , kama tu kipara ni mtindo wa nywele. Naam, hata kipara kinachong'aa cha Didas Ambrozi kilipokelewa vyema na miale ya jua hili lenye hasira punde tu aliposhuka kutoka kwenye gari lake, nje ya mgahawa aliokubaliana kukutana na Bebe. Hofu ya masaibu yaliyomkuta ikaungana na ukali wa jua hili, vikamchanganya na kumkasirisha. Akakunja ndita usoni baada ya kugundua kuwa asingeweza kulitazama jua hili, ili walau alirushie tusi. "Hili jua limetumwa au?" Akalalamika huku akikihifadhi kipara chake kitukufu ndani ya kofia. Akapiga hatua ndefu ndefu na kuingia ndani ya mgahawa ule. Haikumchukua sekunde kumi kabla macho yake hayajainasa nafasi kwenye kona kama alivyokuwa ameelekezwa. Hapa alikuwa ameketi Bebe. Ambaye ameufunika mwili wake gubigubi kwa mtandio, suraye ameipamba kwa miwani kubwa ya jua na kichwa chake kikiwa ndani ya kilemba. Mezani hana chochote kile kinacholika, badala yake ana chupa kubwa ya maji ya kunywa. Ameketi kwa utulivu, mkono wa kushoto umeshika tama na ule wa kulia ukiigonga gonga glasi ile ya kioo iliyojazwa maji. Alifanana na mwanamke ambaye kama hayuko kwenye maombolezo basi alikuwa na lengo lake binafsi. Na kweli, kwake yeye mavazi yote haya hayakuwa na lengo tofauti zaidi ya kuepuka kujulikana na watu, ama kujiepusha na usumbufu usiohitajika kutoka kwa mashabiki zake. Bahati iliyoje, muda huu hapakuwa na watu wengi ndani ya mgahawa. Didas akamfikia na kumsalimia, lakini hakujibiwa. Hapa akagundua tofauti nyingine ya ziada, ambayo ni kama aliitegemea abadani. Bebe hakuwa na furaha. Mhudumu aliyekuwa karibu akaichangamkia meza yao na kumuuliza Disas chakula ambacho anakihitaji kwa mlo. "Nitakuita!" Jibu fupi lilitosha kuuzima ule uchangamfu wa mhudumu yule, ambaye aliificha hasira yake kwenye tabasamu la uongo. Kimyakimya Didas akaketi katika kiti mkabala, akamsogelea kwa ukaribu na kumtazama usoni. Bebe akavuta kamasi puani mwake katika namna ya huzuni, hapa akavua miwani na kutazamana na Didas uso kwa uso. Macho ya Bebe yalikuwa yamevimba baada ya kulia kwa muda mrefu. Walitazamana bila kutamka lolote. Didas akaamua kukohoa kidogo na kuuvunja ukimya, "Nisikilize Bebe...kila kitu kitakuwa sawa. Hauna haja ya kulia na kuhuzunika wakati mimi nipo. Usijali, nitampatia chochote anachokitaka. Kama anachokitaka ni fedha, hilo sio tatizo kwa-" Didas akakatishwa. "Ulivyoongea naye mara ya mwisho amekueleza anachokihitaji?" Sauti ya Bebe iliokata tamaa ikatupa swali. "Uum...yeye nimeongea naye asubuhi hii hii, lakini inaonekana ana kiburi mwanaharamu yule, nitamfanya aju-" Didas aliyeanza kubwata akakatishwa. "Umeshafahamu anachokitaka?" Bebe akarudia swali lile. Sasa ni mtulivu, haonekani kuwa na wasiwasi na wala hana papara katika kuongea kwake. Mchirizi mwembamba wa jasho ukamtambaa bwana Didas kutoka kwenye paji la uso wake, akavua kofia yake na kuwahi kuufuta kabla haujafika kwenye shavu lake la kulia. "Hapana hajaniambia...kanieleza kuwa amekupatia maelekezo yote wewe." Akatamka huku akipambana kupangusa matone yote ya jasho yaliyotia kambi kwenye kipara chake na paji lake la uso. Bebe akashusha pumzi ndefu na kutamka, "Ana mahitaji mawili tu. Na kulingana na alivyodai, anataka yatekelezwe ndani ya masaa ishirini nne kuanzia kesho. Kwa maana hiyo mpaka kufikia keshokutwa, kasema lolote litakalotokea tusimlaumu." Didas akakurupuka na kasi yake ya kupumua ikaongezeka maradufu, "Ana..anataka nini. Niambie Bebe anataka nini?" Akauliza akiwa amemuinamia Bebe kwa ukaribu zaidi. Macho yamemtoka pima yakikagua huku na huko kama kuna wateja ambao wanayafuatilia maongezi yao kwa ukaribu. Bebe akaketi vyema na kuendelea, "Daddy, kama ikitokea hatujamtimizia kile anachokitaka. Basi ujue kuwa huo nd'o mwanzo wa mimi na wewe kupakwa matope. Akheri yangu mimi nisiye na ndugu, lakini jifikirie wewe mpenzi. Mke wako, wanao, jamii inayokuzunguka na mbaya zaidi sifa ya kampuni yetu." Alipofika hapa Bebe akabadilika ghafla na kuwa mnyonge....ule ujasiri wake ukayeyuka ghafla na machozi yakachukua nafasi. "Nisaidie Daddy....naogopa sana. Jina langu limekuwa kubwa! Nafahamika na watu wengi sana. Kama ikitokea akavujisha hizo video, sifa yangu niliyo nayo itakuwa imenajisiwa tayari. Hakuna dili lolote la promotion nitakalolipata!" Akainama chini na kuuficha uso wake ndani ya ule mtandio, akaanza kulia. Didas akasimama mara moja, akaiacha kiti chake na kuketi sambamba na Bebe. Akamkumbatia kifuani mwake na akachukua jukumu jipya la kumbembeleza. "Usilie mpenzi...hili ni jambo dogo sana mbona. We niambie anataka nini, nitajie hayo matakwa yake huyo mjinga mmoja. Nina hela nyingi mimi, hata akitaka nimpe benki nampa!" Didas akatamba. Ni kweli kwake yeye neno fedha halikumtetemesha hata kidogo. Na ni jambo gani kubwa ambalo mtesi huyu angeliomba kama sio fedha? Alijiamini. Sura yake ikingali bado ndani ya mtandio ule, Mdomo wa Bebe ukawa kwenye mapambano makali na pua, iliyojikita kwenye kuvuta kamasi. "Anataka milioni mia." Sauti nyepesi yenye kilio ikatamka sentensi ile ambayo kidogo iliufanya moyo wa Didas uruke mapigo kadhaa. "Milioni mia?!" Haikueleweka kama Didas anauliza kwa kutosikia vyema au anakishangaa kiasi kilichotajwa. Lakini Bebe hakuwa na muda wa kumjibu, yeye akaendelea kuwasilisha. "Kingi...kingineee..." Akarejea upya kwenye kilio. Tena safari hii akalia kwa nguvu zaidi ya mwanzo. Baadhi ya watu waliokuwa karibu na meza yao wakawatazama kwa udadisi. Kijana mmojawapo miongoni mwa wateja akasogea kwenye meza yao na kuuliza, "Aiseee kiongozi, habari yako bwana. Vipi shemeji ana tatizo lolote?" "Ha-hapana kaka...ni kichwa tu kinamsumbua, si unajua tena wanavyodeka hawa heheheh." Didas akajichekesha ili kuonesha kuwa lile halikuwa jambo kubwa. Kijana naye akajichekesha na kuondoka kishingo upande. "Niambie jambo la pili Bebe,niambie..." akamnong'oneza. "Anataka uuvunje mkataba wangu na kampuni yako!" Hali ya hewa ikambadilika Didas ghafla, mijongeo ya viumbe kama vipepeo...ikaanza kupepea tumboni mwake, akahisi utumbo mdogo umechanganyikana na utumbo mkubwa. Taratibu akamuachia Bebe, akakikamata kitambaa chake na kujipangusa jasho lililokuwa likitambaa shingoni mwake. Alichoka! Bebe akajipangusa machozi na kuuibua uso wake uliokuwa umetota kwa machozi. Akamtazama Didas ambaye alionekana waziwazi kuwa amechanganyikiwa. Huenda hoja ya milioni mia haikumbambaisha, lakini hili takwa la pili lilikuwa kama ngumi ya tumbo kwake. "Hivi huyu mshenzi ni nani?!" Didas akanong'ona huku akikiuma kidole chake kwa hasira. "Hawezi kuwa mmoja kati ya wafanyakazi wa ile hoteli kweli?" Aliongeza swali ambalo halikujibiwa moja kwa moja na Bebe. Akashusha pumzi ndefu na kumtazama Bebe. Macho lake safari hii yalivaa utu mpya, hayakuwa yake ya huruma na wala hayakubeba huba. Alimtazama Bebe kwa macho ya tofauti na Bebe akaligundua hilo. "Ni kwa nini kakupatia wewe haya maelekezo na sio mimi? Au kuna kitu unanificha Bebe." Akiwa na macho yanayoonesha wasiwasi, Didas akatupa swali kwa Bebe. "Unataka kumaanisha nini? Kwamba hauniamini ama?" Bebe akajitetea, sauti yake ikapata nguvu kiasi. "Simaanishi hivyo...lakini huenda ikawa hivyo. Hii ni dhania yangu tu." Didas akakoroma. "Dhahania? Didas...hili ni tatizo letu sote. Kwa hio unataka kusema kuwa nimekula njama na huyu mtu, nikatega kamera pale chumbani? Serious..?" Bebe naye akapandisha sauti...ndita zimeuvamia uso wake mdogo. Kitendo cha kuitwa kwa jina lake la kwanza, *Didas*. Kikamshtua sana Bwana Didas, haikuwa kawaida kwa Bebe kumuita jina hili moja kwa moja. Ikawa ni kama wanapandishiana sauti na kuwavutia wateja waliokuwapo mule ndani. Waama walionekana kama watu wa kushangaza sana. Ni dakika moja tu iliyopita, walikuwa wanabembelezana lakini sasa wanalumbana. Didas akainamisha kichwa chake kwa kukiegamiza kwenye viganja vya mikono yake akisikitika. Aliuona uzito wa dunia ukimuinamia moja kwa moja na kumzidia. Hakutegemea kama video ile ama zile kama tu ziko nyinginge nyingi, kuwa zimgharimu kiasi cha milioni mia moja. Hili kwake angelihesabu kama hasara ya kununua kipande cha jiwe kwa kubadilishana na almasi kubwa inayong'ara. Alikuwa tayari kuipokea hasara hii, sio mara yake ya kwanza kukutana na hasara abadani. Japo hii ilikuwa imemtazama moja kwa moja usoni. Lakini hili suala la kukatisha mkataba wake na Bebe, aliliona kama mpango ambao umekaa kimtego. Akiwa na wasiwasi kuwa labda Bebe amemchoka na amekula njama ili akapate malisho mapya katika sehemu nyingine. Wasiwasi wake bado ulikuwa palepale kwenye dhahania. "Nataka kumjua huyu mtu!" Didas akakoroma. "Umjue? Huo muda wa kusubiri mjuane utautoa wapi Daddy? Tuna siku moja tu. Only one day." Kidole chake kimoja cha shahada kinaelea hewani kuashiria namba ya siku iliyobaki na sauti yake nzuri ya kubembeleza inatangaza hofu yake. Vyote kwa Didas wakati huu havikuwa na nguvu yoyote ile. Kidole kile alikiona kama mdomo wa bunduki iliyoshikwa na gaidi. Na sauti ile aliiona kama sauti ya msaliti. "Bebe umenisaliti!" Didas akatamka huku macho yake yakionekana kung'aa kwa machozi yanayolengalenga. Bebe akaonekana kubabaika, hajui amjibu nini. "Sawa nimekubali!" Sauti tatanishi ikakitoroka kinywa cha Didas. "We si unawasiliana naye huyo jamaa sio? Wewe nd'o anayekupa maelekezo yote au sio? Haya mwambie hivi, na mimi nina matakwa yangu hapa. Mwambie nataka nionane naye uso kwa uso. Atapata noti zake anazotaka na mkataba nitauchana mbele yake! Shwaini!" Akasimama kwa ghadhabu na kuivaa kofia yake. Kisha upesi akaondoka hotelini pale akiwa amevimba kwa hasira. Akamuacha Bebe ambaye alichagua kubaki kwenye utulivu. Utulivu ambao huenda aliuhitaji mno kwa wakati huu. Kuondoka kwa Didas kukapishana na hatua za yule yule kijana aliyesogea mezani pale kuwajulia hali wakati ule. Muda huu hakuja kumjulia mtu hali, bali aliketi moja kwa moja kwenye kiti kilekile alichopishwa na Didas. Moja kwa moja akatazamana na Bebe. "Vipi amekubali?" Likawa swali lake la kwanza. "Mh...hapana, bado hajakubali moja kwa moja. Inaonekana ameushtukia mpango wetu, hasa huu wa kuvunja mkataba." Bebe akamjibu kwa utulivu. Sauti yake ikiwa na nidhamu ya hali ya juu. --------------------------- Namna gani hapa! Ina maana Bebe anahusika kwenye hili dili?Na huyu kijana ni nani? Hebu ngoja tuone, ni nini kalamu ya mwandishi itatupatia. Reaction! Reaction! Reaction!.....reaction zenu ni muhimu jama. Bila kusahau maoni kwenye namba 0763204351. Hii itaendelea...

❀️ πŸ”₯ ❀‍πŸ”₯ πŸ₯Ή 11
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
5/20/2025, 8:14:17 PM

RIWAYA; *KIBIRITINGOMA* MTUNZI; *GODLOVE KABATI* KWENDA KWA; *MAJIVU YA FASIHI channel* WhatsApp; 0763204351 ----------------- SEHEMU YA NANE *Yale maovu yote yafanyikayo gizani, huumbuliwa adharani kwenye mwangaza mweupe.* *Ulimwengu umeumbwa katika namna ya ukweli kushinda daima.* *Haijalishi ni kwa wakati gani, kama utachelewa au la.* *Uongo haujawahi kusimama mbele ya ukweli.* *Na hii ni sehemu ya nane* "Naam, kama nilivyokueleza. Tumepokea ofa nyingi za mashirika, kampuni na watu binafsi wanaokuhitaji kwa ajili ya matangazo yao." Bwana Didas akatamka huku akimakinika na baadhi ya nyaraka alizokuwa nazo mkononi. Yeye na Bebe wameshafika nje ya hoteli kuepusha usumbufu wa mashabiki na adha zisizohitajika. "Na kama ujuavyo, wewe sa'hivi ni mtu huru. Unayo maamuzi ya kufanya kitu chochote unachokitaka. Haya, kuna hizi hapa..." akamkabidhi nyaraka zile ili azisome. Bebe akazipekua upesi upesi bila kuzitilia maanani. Akatabasamu na kutikisa kichwa katika namna ya kukubali. "Ni sawa tu Daddy. Sina pingamizi!" Akazipanga na kumrudishia bwana Didas. "Ina...ina maana umekubali au? Ume...umezisoma zote kweli?" Didas akahoji kwa kubabaika. "Sasa kwa nini nikatae? Maana hapo kwenye kila ofa kuna malipo mazuri. Na hili ni suala litakalotufaidisha sisi sote, mimi na kampuni." Bebe akamaliza kwa kutabasamu. Tabasamu lililomuambukiza Didas, naye akatabasamu pia, tabasamu la kuigiza lililoambatana na wasiwasi. Alichokitamka Bebe kilimuonesha waziwazi, faida iliyokuwa mezani mara tu Bebe atakapokodiwa na kampuni nyingine kutoka kwao. Hofu aliyokuwa nayo ni endapo tu Bebe atapata ofa kubwa zaidi itakayomtangazia malipo ya kiwango cha juu kuizidi kampuni yake. Huenda huo ndio ukawa mkono wa kwa heri kwake na akampoteza Bebe moja kwa moja. Tabasamu lake likayeyuka mara moja alipolifikiria hili. Akahamishia macho yake kwenye zile karatasi na barua zilizokuwa mkononi mwake. Akajitia kuzisoma upya...akatishika. Hakika kurasa za mikataba hii zilifoka utajiri wa pesa za kutosha. Pesa zenye uzito wa kupasua mizani. Ni kweli kampuni ingefaidika kama tu Bebe akikubali ofa hizi, lakini kwake yeye hakuwa na hitaji la pesa wala utajiri. Hivi ni vitu alivyojenga navyo urafiki tangu zamani. Anataka nini sasa? Jibu lake likawa jepesi tu...Bebe. Huyu hapa aliye mbele yake. Alitamani amtunze na awe karibu yake daima! Na hapa akayarudisha upya macho yake usoni kwa binti huyu mrembo aliyekuwa bado ana cheche za lile tabasamu lake. Didas akatabasamu upya na kutamka, "Nakupenda sana Bebe!" Zile cheche zikasuguana na kuunda moto mpya wa tabasamu usoni kwa Bebe. "Nakupenda pia!" Akamjibu na kumsogelea karibu zaidi. Wakakumbatiana na papi za midomo yao zikagusana, Zikaruhusu ndimi zao kupinduana, Wakajitahidi kujizuia, si wakashindwa bwana! Joto la miili yao likapanda bila hiyana, Kila mtu na ashiki yake, tayari kupambana, "Si hapa Daddy..." Bebe akamsukuma kwa upole. Huku akiyalegeza macho yake. Jasho lilianza kumvuja Didas akiwa anahema juujuu. Macho yake yanapepesa huku na kule, wasiwasi na aibu vimemvamia kwa nguvu. "Hii si hoteli hii? Ngoja nikalipie chumba." Akajiwahi. Haooo....wakazama ndani ya hoteli ya nyota tano. Ikamlazimu Didas ateketeze mamilioni ya fedha, kwa ajili ya burudani ya usiku mmoja tu akiwa na Bebe. Madaraja ya maisha! ------------- Akiwa mbele ya kompyuta yake ndogo, J4 alikuwa makini sana na kila kitu ambacho kilikuwa kinaendelea kwenye skrini ya kompyuta hii. Sikio lake linayanasa mawimbi ya sauti na macho yake yana na umakini mkubwa kuzitazama picha zote anazoweza kuziona mbele yake. Mkono wake wa kushoto ulikuwa na kalamu na kando yake palikuwa na kidaftari kidogo alichokuwa anaandika kila taarifa aliyoipokea na kuipa umuhimu katika shughuli hii. Ni shughuli gani? Anajua mwenyewe. Mara anakunja ndita na kuihamishia kalamu ile mdomoni kwa dakika kadhaa. Kisha anaendelea kuandika. Ghafla simu yake ya mkononi ikaita. Jina la aliyempigia lilisomeka kama D, akatabasamu. Ni yuleyule swahibu wake mkubwa- Dotto. Kabla hajaipokea, akasimamisha shughuli zake kwenye kompyuta, alimuelewa sana huyu rafiki yake. "Kama hana mchongo wa hela ya haraka huko kwenye ulanguzi wake huyu....basi ni wanawake." Akawaza na kuipokea upesi simu ile. Kama kawaida zikaanza salamu zilizoambatana na matusi ambayo daima yalinyimwa uzito wa kuitwa matusi na yakapewa uzito wa salamu ya kawaida. Maongezi yao yakaendelea kisha mara D akauliza swali ambalo lilimrejesha J4 kwenye uso wa kompyuta ile. "Vipi kuhusu yule demu wako mzee...umefikia wapi sasa?" "Duh kaka, kuna ramani moja kali ninaichora hapa, yule atanasa tu. Hutaamini bro, we tulia!" J4 akarekebisha upya video zake alizokuwa akizitazama pale kwenye skrini ya kompyuta yake. "Aah wapi, wewe mzito sana mdogo wangu ile pisi ni ya viwango vya kimataifa!" D akatania huku akitokwa na cheko la dharau. "Hautaamini bro...nitakushangaza!" J4 akamjibu huku akiwa bado anapekua faili ambalo alikuwa liliuvutia umakini wake. "Yule ukimpata nitatembea uchi mitaa yote ya Manzese." D akatamba. "Hebu sikilizia kwanza bro...kata simu chap! Kuna kitu hapa nimekiona!" J4 akamshtua D. "Umeona nini dogo? Umeo-" Alikuwa suala la kusubiri simu ikatwe, akaikata mwenyewe. J4 akainama na kuitazama skrini ya kompyuta ile kwa umakini zaidi, kuliko ule wa awali. Lilikuwepo faili la video ambalo alikuwa analisubiri kwa muda mrefu. Akalifungua. Hamadi! Alichokiona kilimkurupua mara moja kutoka kwenye kiti chake. Akasimama na kutupa ngumi ya ushindi hewani. Huenda huu ulikuwa ni wakati bora zaidi aliokuwa akiusubiri kwa hamu kubwa. Upesi akarejea kwenye kompyuta yake na kucharaza maneno kadhaa ambayo yalilihifadhi faili hili kwa upekee wake peke yake. "Nitawashangaza!" Akatamka na kucheka kwa sauti. Sauti iliyopenya kwenye giza la chumba kile chenye mwanga hafifu, ikadunda kwenye kuta na kuishia mulemule chumbani. Ni siri yake. -------------- Ilikuwa ni siku njema iliyoanza kuonekana tangu asubuhi kama wasemavyo wahenga. Haikuzoeleka hivi kwa Bwana Didas hata kidogo. Asubuhi hii aliamshwa kwa upendo na mke wake wa ndoa, akaandaliwa chai nzito ambayo alishiriki pamoja na familia yake mezani. Mkewe akamkumbusha kuwa bado anampenda. Akambebea briefcase lake mpaka kwenye gari, kisha akamuaga kwa busu zito na kumbato la huba. Ajabu hii! Hivi vitu mara ya mwisho kufanyiwa na mkewe hakumbuki ilikuwa ni lini...ama yeye mwenyewe aliruhusu atendewe hivi lini? Hakumbuki. Alizoea kulumbana na mkewe, hakuwa na muda wa kukaa na familia yake. Daima alidai kuwa amezikumbatia shughuli za ofisini ili ailishe familia yake. Sasa mambo yalikuwa yametakata, madirisha ya neema yamemfungukia na maendeleo yanagombana kuishi naye. Didas akameza funda la mate na kuondoka akiwa mchangamfu mno. "Kuna nini leo?" Alijiuliza. Hata barabarani hakukuwa na foleni kama alivyotarajia. Akafika ofisini mapema, yeye kama mkurugenzi siku hii akawa mfano bora wa kuigwa. Alifika hata kabla ya karani wake. Siku hii hakuwa na mafaili ya kushughulikia zaidi ya kusaini fedha kadha wa kadha zinazoingia kama faida. Ilikuwa ni zaidi ya neema. Bwana Didas akafumba macho yake na kutabasamu. Kila alipoyafikiria mafanikio, jina Bebe likatangulia. Bebe alikuwa ni ufunguo wa kila kitu alichokuwa akihitaji kwenye maisha yake. Akasimama na kutoka nje ya ofisi yake, akahesabu hatua zake akiwa mwingi wa furaha mpaka kwenye roshani iliyokuwa katika ghorofa ile. Hapa aliweza kuyatazama majengo kadhaa ya jiji la Dar es Salaam na pilikapilika zilizokuwa zinaendelea ndani yake. Akaifikiria fahari yake iliyomjia katika namna ya ajabu na haraka tangu amemfahamu Bebe. Akiwa kwenye fikra hii, simu yake ikaita na alipoitazama ilikuwa ni namba ngeni iliyompigia. Akafikiria kuipuuza lakini akachelea kuwa huenda ni mteja ama ofa mpya inabisha hodi. "Namna gani bwana...mbona namba ya simu ya mezani inajulikana? Eboh!" Akasonya na kuipokea akiwa amekunja sura. Hakuzungumza kwanza, akasikilizia upande wa pili uliopiga. "Bwana Didas habari yako!" Ilikuwa sauti ya kiume, iliyojaa ubichi. Angeweza kuidai salamu kama akitaka. "Salama! Naongea na nani?" Akajibu kwa kifupi. "Utanifahamu tu kiongozi wala usiwe na haraka. Nina ujumbe wako tu hapa, ambao-" akakatishwa. "Mimi unanifahamu hongera kwa hilo. Lakini mimi bado sijakufahamu. Kama huwezi kujitambulisha sina haja ya kuzungumza na wewe!" Akataka kukata simu lakini akagundua kuwa hawezi kuikata. "Taratibu kiongozi taratibu...haya maongezi ni yangu mimi na wewe tu. Hakuna mtu anayesikia wala anayeweza kuyafikia, kuwa na amani kabisa." Sauti ile ya kijana wa kiume ikarindima. "Wewe ni nani kijana?" Didas akauliza baada ya kuona jitihada za kukata simu ile zimeshindikana. "Utanifahamu hivi punde tu wala usijali. Hii simu huwezi kuikata, unachotakiwa kufanya sasa hivi ni kufungua mtandao wako wa WhatsApp na kutazama ujumbe niliokutumia. Baada ya hapo nitafute kabla ya adhana ya saa saba! Shime.." Simu ile ikakatwa. "Kelbu!" Didas akarusha tusi. "Hii mihadarati na bange vitakuja kutuharibia taifa." Akaweka nukta. Moyo wake ukadunda kwa nguvu baada ya kukumbuka maelekezo aliyopewa. Upesi akaingia katika mtandao wa WhatsApp na kupekua jumbe kadha wa kadha zilizoingia hivi punde. Kweli, akaona ujumbe kutoka kwa namba ngeni. Akaufungua! Lilikuwa ni faili dogo tu la video lililoambatana na ujumbe, "Hiki ni kipande kidogo tu cha keki nzima!" Akaufungua ujumbe ule. Ilikuwa ni video...mara ghafla zikasikika sauti za miguno ya mahaba! Akapunguza sauti ya simu upesi akihofia sauti ile kusikika na watu. "Kijana mjinga sana huyu, anafikiri kila mtu anapenda hizi video za uchafu?" Akatazama vizuri, ilikuwa ni video iliyounganishwa katika namna isiyoeleweka kamera ilikuwa upande gani. "Kina nani hawa?" Akakaza macho yake. Alikuwa ni yeye na Bebe. ------------- Nimekuwa bize kidogo wakati huu... Lakini hakuna kitakachonizuia kuitumikia fasihi. Tusiache kusambaza link ya chaneli yetu. Itaendelea Alhamisi

Post image
❀️ πŸ‘ πŸ™ ❀ 8
Image
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
2/19/2025, 5:22:18 PM

*`SHAMBA LA HELA`* Yake; *Godlove Kabati* WhatsApp; 0763204351 ------------------------------- SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU *`BADO MASAA MAWILI...`* --------------------------------- Franko Don Bosco, ama Don Franko; Alikuwa ndani ya chumba chake kidogo ambacho yeye alikiazima imani yake yote na kukichukulia kama ofisi. Akiwa amesimama anazunguka zunguka huku na kule, kichwa chake kikipanga mawazo na kuyapima kisha kingeyapindua na kuyakataa. Halafu angepanga mengine na kuyaona yako sawa akayakubali. Mara likaingia wazo jipya lililomsogeza moja kwa moja mpaka juu ya ukuta ambapo alikuwa ametundika picha moja kubwa. Akaisogelea taratibu na kuikazia macho. Ilikuwa picha ya mtu ambaye kwake daima alikuwa ni adui namba moja. Kila alipoiona picha yake, aliitukana na kuinuzia laana na maneno yote mabaya aliyoyafikiria. Alimchukia mno! Na hii nd'o sababu akaitundika picha ile pale ukutani akaifanya kama kumbukumbu itakayoweza kumkumbusha jukumu la muhimu mno ambalo anadaiwa yeye kama kiongozi wa chama hiki cha siri. Akaitungua picha ile kutoka pale ukutani akaiweka mezani. Akaiinamia huku akiitazama upya kwa jicho makini zaidi. "Dario!!" Akalitaja jina la taswira aliyoina pale juu ya picha. Akiwa mwingi wa hasira na uchungu, akayafumba macho yake na kukumbuka kila tukio ambalo Dario alifanya na likamuumiza huko nyuma. Yeye akiwa bado hana cheo chochote kile ndani ya hiki chama, japo ana uzoefu na utumishi wa muda mrefu. Akaikumbuka ile siku ambayo wanampokea rasmi Dario kama kijana mdogo tu, akakaribishwa na kula viapo vyote. Kwa wakati huo, Dokta Albert Simfukwe ndiye alikuwa mkuu wa chama. Akakumbuka jukumu walilopewa yeye na Dario, kwenda kuuondoa uhai wa aliyekuwa Raisi wa nchi kwa wakati huo, ambaye alikuwa amejenga vizingiti vilivyowazuia kufanikisha biashara zao. Akaukumbuka uzembe ambao yeye aliufanya mpaka akakamatwa huku Dario akigeuka shujaa baada ya kutumia mbinu yakinifu na kufanikisha mauaji hayo. Kwa mara ya kwanza kabisa, Dario akakwezwa na kukaa kiti cha juu kuliko yeye. Kisha baada ya muda mfupi tu, akaaminiwa na kupewa fimbo ya mamlaka iliyomvesha cheo cha uFranko. Cheo kikubwa ambacho kinamilikiwa na watu watano tu ndani ya chama. Eti na yeye akakinyakua cheo hicho kiulaini kabisa. Ikawa ni kwamba DonBosco anapokea amri ma maagizo kutoka kijana kama huyu, ambaye amemtangulia idadi ya vikao vya chama. Kwake huu ulikuwa uonevu mkubwa. Akakumbuka namna ambavyo, huyuhuyu Dario alimuua mkuu wa chama, Dokta Simfukwe kisha akatoroka na kujificha pasipojulikana akiwa na faili lenye siri kubwa ya utajiri wa chama hiki. Akaondoka na kuliacha ghala lao likiwa jeupe. Akafumbua macho yake baada ya kugundua kuwa ni leo wanaenda kumtia mbaroni na kurejesha nguvu ya chama chao ambacho kilikuwa kimeanza kuipoteza nguvu yake baada ya kukosa nishati ya fedha na utajiri. "Mpumbavu wewe...fidhuli mkubwa! Mjaa laana na hayawani! Hivi ilikuwaje mpaka ukaingia kwenye chama chetu?" Ilikuwa ni kama anazungumza na ile picha moja kwa moja. Anaitukana lakini haionekani kuumizwa kwa matusi yale, anaiuliza swali lakini hajibiwi. Badala yake ikabaki kumtazama tu, tena miongoni mwa macho yaliyomtazama lilikuwepo lile jicho bovu lililokuwa na kovu kubwa lililotengeneza mpasuko katikati yake. Tabasamu kavu likiuvaa uso huu na kuifanya sura ile kufanana kwa ukaribu zaidi na sura ya shetani asiyeuogopa moto wa jehanamu. Ni tabasamu hilo lililomfanya Don Franko atishike kidogo na akaitupa mbali picha ile ikadondoka sakafuni. Na ikapata mpasuko kwenye kioo ambao ulitengeneza ufa uliokatiza pale pale kwenye kovu la sura ile! "Huwezi kufa hata kwenye picha?!" Don Franko akaunguruma kwa hasira. Akakusanya nguvu zake zote na kutungua kisu kikubwa cha kijeshi kilichokuwepo palepale ukutani. Kisha akakikita kwa hasira juu ya ile picha. Akarudia rudia kuchoma picha ile kwa kisu mara kadhaa mpaka alipotosheka kuwa kioo kimesagika na picha imeharibika barabara. Akatoa tusi kali mno, akiukashifu uchi wa mama aliyemzaa Dario. Akiwa bado hajazinduka kwenye wazimu wake, mlango wa chumba chake ukafunguliwa na akaingia mwanamke aliyevaa mavazi yaliyoshabihiana na ya kwake, Franko Viktoria. Hakumpa muda wa kushangaa au kuhoji ni kitu gani kinaendelea pale ndani, "Kila kitu kiko tayari?!" Kwa sauti inayotetemeka Don Franko akamuuliza. "Ndio...nimeshakamilisha kila kitu." Akajibiwa kwa sauti ya kike iliyokuwa na kila dalili ya kujiamini japo usoni alionekana mwingi wa maswali. "Vizuri. Nadhani mkae sawa,leo saa kumi na mbili jioni tutaanza safari" akatoa amri kisha akageuka na kuketi juu ya kiti huku jasho likimtiririka. "Mkuu una uhakika uko sawa kweli?.." Viktoria akamuuliza huku akitupa macho yake kwenye sakafu iliochafuliwa kwa vipande vya vioo. Hakujibiwa mpaka alipouliza swali hili mara mbili. "Ni muda mrefu sana tangu nilipopania kumkamata huyu hayawani. Na sidhani kama kuna kitu chochote kile ambacho kitanizuia kumharibu!" Akauma meno yake kwa hasira. Kisha akatazama saa yake ya mkononi, "Tumebakiwa na masaa nane tu!" Kauli yake ilieleweka na ikamuondoa Viktoria kutoka pale chumbani. ******* Mnamo majira ya saa kumi jioni, ugeni mpya ambao haukutatajiwa uliwasiri mbele ya jumba hili kubwa lililofanana na kasri. Gari aina ya VX lilizuiliwa na walinzi ambao daima walikuwa makini kuchambua magari yanayoingia na kutoka kwenye uzio huu. Na yeye wakazuia gari lake lisipenye katika geti la jumba hili. Aliyekuwemo ndani yake akafoka na kulalamika kama ambavyo alizoea kufanya hivi siku zote. "Namna gani bwana! Kijana...mimi ninaweza kukufanya uachishwe kazi hapa! Usiniletee upuuzi wako!" Alifoka kwa sauti kubwa. Walinzi wale ambao walisimamia kauli yao kuwa hakuna mtu yeyote yule aliyealikwa siku hii na hawana maelekezo ya kumruhusu yeyote wakazidi kutanua vifua vyao kumzuia asipite. Akatoka nje kwa hasira akiwa amechachamaa! Akatoa simu yake mfukoni na kuipekua upesiupesi huku akiendelea kutukana. "Mnajifanya mnajua sana sheria eh?! Sasa ngojeni!" Akainyanyua mpaka sikioni mwake ikiwa inaita. "Halooo! Naam Franko!...kama nilivyokueleza. Naona hawa mburukenge wananizuia nisipite hapa!" Akafoka! Kelele zake zikawachangamsha mpaka mbwa ambao walikuwa wakishikiliwa siku zote kusaidia ulinzi na kukosa kazi maalumu maana hapakuwa na hatari yoyote ambayo wangeishuku. Leo hii wakaona fursa ya kuonesha umuhimu wao na ili waonekane kuwa hawali nyama za bure, wakaanza kubweka kwa fujo. Mara moja simu ikapigwa na maelekezo mapya yakatolewa. Ishara zikatembea baina ya hawa walinzi na wakachungulia ndani ya gari lake kuhakikisha kuwa alikuwa ni yeye peke yake kisha geti likafunguliwa kumruhusu mgeni huyu aingie. Akarudi ndani ya gari mara moja huku akisonya kisha akavurumisha gari lake kwa fujo na kuzama ndani ya uzio huu mkubwa. Nyuma yake geti likafungwa na ukimya ukarejea upyaa. ******* "Unataka kuniambia kuhusu nini?" Don Franko akamuuliza Brown Kizito, Boss Mzito! Mgeni ambaye ni nusu saa tu iliyopita tangu wawasiliane na kumruhusu afike mahala pale kabla hajakutana na rabsha za walinzi kumzuia getini. Akakohoa kidogo na kutamka, "Najua kuwa leo nd'o siku iliyopangwa kwenda kumuwinda huyo mbaya wetu hukohuko alikojificha na mimi kama mtu wa karibu nisingekubali kuliruhusu hili lipite bila kuweka walau thumuni ya jitihada zangu kukisaidia chama chetu!" Akaweka pumziko kisha akaendelea. "Nimekuja hapa ili kukupa dondoo kadhaa juu ya huyo mtu mnayeenda kumtafuta leo hii. Kwanza kabisa naomba unipe ruhusa yako...kabla sijaendelea!" Akainamisha kichwa chake kwa nidhamu. Don Franko akarekebisha mkao wake juu ya kiti akapumua pumzi ndefu kisha, "Endelea Kizito...endelea!" "Naam, ujue mtu tunayeenda kumtafuta huko hatujui ni namna gani amejipanga! Na isitoshe sisi hatuna ramani ya ule msitu. Naogopa sana kudhania kuwa tunaenda kupigana vita kwenye uwanja wa ugenini. Tena tunaingia kichwakichwa tu bila ya kuwa na uelewa mzuri wa mitego ambayo tumetegewa huko!" Akaweka kituo akimtazama Don Franko, akiwa na matarajio kuwa maneno yake huenda yatamfurahisha ama yatampa sifa kubwa. Badala yake Don Franko akaangukia kwenye kicheko cha kifidhuli ambacho kilimfanya apaliwe na kukohoa kwa taabu kwa sekunde kadhaa. "Sikutegemea kama utafikia hatua ya kutudharau namna hii Brown, sikutegemea kabisa! Yaani ni heri maneno uliyoyasema nimeyasikia mimi peke yangu. Maana nina uhakika kama timu yangu yote ingeyasikia basi muda huu wewe ungekuwa umepasuliwa vipande vipande halafu mbwa wa kule getini wangeachiwa nyama yako wakufaidi! Yaani unadhani sisi ni wapumbavu kiasi hicho? Kweli Brown?" Akabadilika sura yake na akavaa uso ulioiva wenye macho yenye gadhabu. Brown Kizito, a.k.a Boss Mzito akajichekesha na kutamka, "Aaah hapana mkuu kwani kuna jambo ambalo sijalijua? Au nipo nyuma ya muda kidogo" Don Franko akasikitika kisha akanyanyua kichwa chake na kumtazama upya Kizito, "Ni nani aliyekuroga? Ulianza vizuri sana lakini naona unazidi kupungukiwa na akili siku baada ya siku. Hivi unadhani sisi tunaweza kwenda vitani bila kujua tunapigana na nani?! Nakusikitikia sana ndugu yangu, mchawi aliyekuroga siku hizi hajaondoka na akili tu, amekokoroa mpaka ufahamu wa kawaida ambao kila mtu anao. Hata hivyo sishangai... Ni upumbavu wako huohuo uliotufelisha kumkamata huyu kijana upesi, eti ukakodisha vijana wa mtaani licha ya ukwasi ulionao. Ni upumbavu huohuo unaokufanya ugombane na walinzi getini. Kamuombe msamaha huyo mchawi aliyekuroga! Mwambie akurudishie walau robi ya ufahamu wa kawaida!" Akamaliza. Boss Mzito akakohoa kidogo kisha kwa sauti iliyojaa nidhamu akajititumua na kutamka, "Uum mkuu! Sio kwamba nina hofu juu ya utendaji wenu na mipango mlioiandaa. La hasha! Nilichokitaka mimi ni kushiriki bega kwa bega na nyinyi kwenye hii shughuli. Nataka nipigane pamoja nanyi ubavu kwa ubavu. Mpaka tufufue kila kitu ambacho chama chetu kimepoteza. Hilo tu!" Akanyanyua mikono yake kama ishara ya kusihi na kujiondoa kwenye upande wenye makosa. Boss Mzito akatazama saa yake ya mkononi kisha akasimama na kuondoka bila kumtazama Boss Kizito huku akisema, "Tuna masaa mawili tu! Kaa tayari..." Akamuacha Mzito pale juu ya kiti. Na alipotoweka usoni mwake, Boss Mzito akakagua pembe za chumba hiki kikubwa na akang'amua kuwa hakukuwa na kamera wala rwkoda zozote zile zilizokiwa zikimtamzama. Akavuta kifaa kidogo kilichokuwa kwenye kifungo chake cha shati akakibofya na kutamka... "Nadhani mmesikia kila kitu....saa kumi na mbili kamili wataondoka hapa rasmi. Kaeni tayari!" Kisha akakibofya kukizima. Akasimama na kuondoka eneo lile kimya kimya. ******* Ndani ya buti ya gari lililoingia punde tu ndani ya uzio wa jengo hili, kulikuwa na viumbe wawili ambao jasho liliendelea kuwavuja huku joto likifukuta kwa fujo. Taarifa ya kuendelea kusubiri kwa masaa mawili zaidi, ikawafanya wajutie mpango huu waliousuka wao wenyewe. 'Tutakuwa kwenye buti ya gari yako na usifanye upuuzi wa aina yoyote ile tutawashtua wenzetu ambao wanatufuatilia kila hatua ambayo tunapiga na wewe! Wewe fika huko na hakikisha tunafika mpaka eneo la tukio!' Yalikuwa maelekezo maalumu yaliyotolewa na Konstebo Tito Ngeze ambaye muda huu alitaka ajulikane kama nabii Tito kwenye hii misheni. Boss Mzito akatii na kuhaidi uaminifu wake endapo tu ataokoka na mikono yake ibaki safi. Abednego Kagoye akaongezea kitisho kuwa kama akiwachomea utambi kwa hawa matajiri wake basi na yeye ataweka wazi kila siri aliyoitoa. Huyu akataka kujulikana kama Kingi Nego kwenye hii misheni ya kumuokoa swahiba wake Feruzi. Wakala dili na sasa yamebaki masaa machache tu. ---------------------------------- Naam bado masaa mawili.... Timu mbili zimejiandaa kwa ajili ya mapigano.. Don Franko dhidi ya Franko Dario. Kitajiri nini tena huko msituni? Haya yote tutayajua hapa hapa... Muhimu share link ya chaneli *`ITAENDELEA KESHO`*

πŸ‘ πŸ’ͺ 2
Image
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
MAJIVU YA FASIHI. πŸ“–πŸͺΆ
2/7/2025, 8:37:12 PM

*`SHAMBA LA HELA`* Yake; *Godlove Kabati* WhatsApp; 0763204351 -------------------------------- SEHEMU YA KUMI NA TISA *MWANGA WA GIZA* ---------------‐------------- "Naam...ni mimi!" Mtu huyu mgeni aliyeingia ndani ya chumba pasi na kujulikana alikotokea akamjibu kwa sauti ileile iliyokauka. Feruzi akatamani kuparamia ukuta atafute upenyo na akimbie lakini akagundua kuwa akifanya hivyo ataishia kuchekesha tu. Akajua kuwa yuko mbele ya mzuka wa Mtemi, rafiki yake ambaye siku mbili au tatu nyuma aliambiwa kuwa ameagana na uso wa dunia. Lakini muda huu huyu hapa, anatazamana naye. Akamkagua kuanzia juu mpaka chini...akatambua mara moja kuwa mwili wa Mtemi ulimdhiaki kwa kupoteza gramu nyingi sana ndani ya siku hizo alizopotea na kumfanya aonekane kuwa amedhoofu. Alikuwa na michubuko kadhaa kwenye uso wake na mavazi yake yalikuwa machafu sana na ilionekana kuwa amejenga urafiki mpya na vumbi aidha kwa kugaragara mavumbini au kuoga mavumbi halafu akaanzisha uadui na maji. Kimsingi alifanana na mtu ambaye ameokotwa vitani kisha akatupwa uraiani na kutelekezwa aitafute amani yake yeye mwenyewe. "W-we..wewe ni nani aisee?" Kwa woga akauliza akijitahidi kukaa mbali iwezekanavyo kutoka kwa huyu Mtemi mpya aliyefufuka na kuja hapa mbele yake. Huyu hakuwa Mtemi aliyemfahamu. Huyu alifanana na chokoraa. Swali lake halikujibiwa. Akahamishia macho yake kwenye miguu yake, mguu mmoja ulikuwa peku na mwingine uliruhusu kidole gumba kichungulie nje baada ya kutobolewa kwenye namna isiyoeleweka. Hali yake ilitisha sana. "Umekuaje wewe? Nini kimekukuta mzee? Kwanza ulikuwa wapi..." Mvua ya maswali ikamnyeshea Mtemi. Mtemi hakumjibu moja kwa moja kwa matamshi. Badala yake akatikisa kichwa chake kwa huzuni kisha akatamka kwa sauti ya chini, sauti ya unyonge ... "Nisikilize Feri..." Akatulia kuvutia usikivu wa Feruzi kisha akaendelea huku akipiga hatua kumsogelea kwa ukaribu, akagundua kuwa naye Feruzi alijitahidi kusogea mbali naye kadri awezavyo kwa maana alimuogopa, "Mimi sio mzimu...na wala sikufa kama ulivyoambiwa na Franko Dario! Kwa hio usiniogope.Bado naishi kaka....Lakini maisha yangu ni kama nimeyalipia kuponi. Kila ninapoenda inanibidi niwe nayo ili nizidi kupumua!" Sentensi zake tata zikazua maswali lukuki kwenye kichwa cha Feruzi, ambaye naye hakusita kuyatapika muda huohuo, "Kuponi?! Mbona sikuelewi....na huyo Frenki sijui Franko Daaario ni nani huyo?!" Mtemi akamsogelea kwa karibu zaidi huku akichechemea na kabla hajamfikia akaganda kwa sekunde mbili akiwa ameshikilia tumbo lake, akakunja uso akiashiria maumivu makali. Kisha akamtazama Feruzi, "Hatuna muda mrefu sana wa kuzungumza bro...mimi nimeletwa hapa kama ulivyoletwa wewe. Na hawa watu tutakaokutana nao leo hapa ni watu makini sana ambao hawashangai kuona damu inavuja. Kwao kuua ni ibada!" Maneno yake yakazidi kumchanganya sana Feruzi. "Oyae! Hebu sikia...ina maana na wewe umeletwa hapa na huyo jamaa mwenye kovu usoni au?" Kwa sauti yenye jazba kidogo akalalamika. Mtemi akiwa bado ameshikilia tumbo lake akatikisa kichwa chake kwa huzuni kwa mara nyingine kisha akamtazama Feruzi, akamuinamia na kutamka kwa sauti ya kunong'ona, "Sikia bro....hapa tumetekwa. Na waliotuteka sio huyo jamaa unayemuongelea wewe. Hawa ni watu wengine tofauti kabisa!" Akamjibu. Feruzi akahisi kama mwili wake unaanza kuchemka, joto likampanda na picha za kumbukumbu zikaanza kujijenga kwenye ufahamu wake. Akakumbuka namna alivyokuwa anatafutwa na watu wasiojulikana huko mtaani kwake na sasa huenda ndio hawa hawa wamempata. "Hawa ni kina nani?! Askari au?" Akamuuliza vilevile kwa sauti ya kunong'ona. "Ni heri basi hata wangekuwa ni askari! Hao watakusumbuasumbua..halafu wakusweke rumande, ukiwapa shilingi kadhaa wanakuachia. Lakini hawa ni watu wa kikundi hatari! Nimeambiwa machache tu kati ya mengi yao, na nikaridhika kuwa naenda kukutana na changamoto mpya!" Akamjibu. "Nani amekwambia huyo?..." Feruzi akazidi kuuliza. Maswali yake mengi bado hayajajibiwa. "Franko Dario!" "Ni nani huyo?" "Yule jamaa uliyekutana naye porini yule...akakuachia uende bila kukuhangaisha! Mshukuru sana, alikufanyia upendeleo wa hali ya juu." Mtemi akamjibu na kisha akaongezea, "Ilaaniwe sana ile siku ambayo nilikupatia pikipiki yangu ukaenda kumpakiza yule kiumbe...kama ningekuwa na uwezo hata ile tarehe ningeifuta kabisa kwenye kalenda! Nisikilize rafiki yangu... Nimekutana na watu wa ajabu sana. Sijui ni lugha gani ile wanazungumza. Ni kama wamejitungia lugha yao huko porini. Wanaijua wao! Tamaa yangu ilinisindikiza kwenye mdomo wa mauti, halafu ikaniacha niangamie kabla hata sijamezwa na mdomo huo wa kutisha. Ulifika muda ambao mimi mwenyewe nilikiomba kifo, nikakitamani kifo kwa uchu mkubwa sana. Sikujua kama haya yote yatatokea asilani. Bro..nimepigwa kila aina ya kofi...sikuwahi kuzimia tangu nizaliwe lakini kule porini nimezimia zaidi ya mara kumi. Nimelazimishwa kula ugali mkavu bila mboga wala maji ya kunywa na nilipogoma nikalazimshwa kutafuna ulimi wangu kama mboga." Feruzi akaonekana bado ni mwingi wa maswali na hofu. Akatazama huku na huko kisha akamtazama Mtemi tena, "Enhe kulikoni tena imekuaje uko hapa kama alikuwa bado amekushikilia?" Kabla hajajibiwa, wakakurupushwa baada ya mlango wa chumba kile kilichofanania na ukumbi mdogo kufunguliwa. Kikaingia kikosi cha watu saba ambao walivaa suti nyeusi na wengine wakaongezea makoti makubwa juu ya suti hizo. Miongoni mwao walikuwepo wanne ambao mikono yao ilimiliki fimbo zilizogusa sakafu baada ya kila hatua wanayopiga. Walionekana kuwa ni kikundi maalumu chenye utaratibu wa pamoja au ni chama fulani. Waliingia moja kwa moja huku wakiwatupia macho Feruzi na Mtemi waliokuwa wamesimama. Bila kuuliza chochote wakachukua nafasi zao kwenye viti vilivyokuwepo ndani ya chumba kile. "Jamani karibuni mketi...miguu yenu isije kuingia tumboni aisee, mmesimama muda mrefu sana!" Mmoja kati ya watu wale akawasogezea viti viwili Feruzi na Mtemi ili waketi. Wakatii na kisha kwa kusita wakaketi huku wakiwa na hofu ya ni nini kitafuata baadaye. Feruzi akaamua kuwakagua hawa watu waliowazunguka, yeye na Mtemi wakiwa katikati ya ukumbi huu mdogo. Ni watu wasiowafahamu, watu waliovaa mavazi meusi kuanzia juu mpaka chini, nguo mpaka viatu. Ilionekana kama dhambi kuvaa vazi lolote lenye rangi tofauti na nyeusi. 'Kina nani hawa?' Alijihoji. "Naitwa Franko Don Bosco ama ukipenda waweza kuniita Don Franko, nitafurahi pia. Na hawa ni wenzangu kazini, sitaki kupoteza muda kuwatambulisha mmoja mmoja. Lakini sisi ni wanachama wa chama kimoja. Mwanga wa giza!" Akatamka na kuweka kituo, akaacha maneno haya yazame kwenye akili zao. Kisha akaendelea, "Uuum sisi ni watu wema sana, japo tuna tabia moja mbaya ambayo hata sisi inatushangaza pia. Tunabadilika haraka sana, yaani hasira zetu huwa tunakaa nazo jirani tu. Zinakuja bila kualikwa! Lakini ni kama tu tukivurugwa." Sauti yake nzito iliorindima ndani ya chumba kile chenye ukimya, ikamfanya Feruzi ameze mate kwa woga. Mtemi alikuwa bado amelipakata tumbo lake na ametazama ardhini. Ni kama ambaye hana habari na kinachoendelea. Hata wale wanachama wengine walikuwa watulivu na hawatikisiki ni kama ambao wanaimba wimbo wa taifa. Wengine waliovaa miwani nyeusi kuficha macho yao ndio kabisaaa walifanana na sanamu. 'Mwanga wa Giza!' Ndio neno lililoendelea kupiga honi kwa nguvu masikioni mwa Feruzi. "Mnataka nini kutoka kwetu? Na tumewakosea nini..." Feruzi akajitutumua na kuuliza swali. "Umeuliza swali sahihi sana kijana...lakini haujaliuliza kwenye wakati sahihi." Akaweka pumziko kisha akaendelea, "Waungwana tunatambulishana kwanza bwana...mimi mmenifahamu lakini nyie siwafahamu." Donge kubwa la hasira likajikita kwenye kifua cha Feruzi. Kutekwa na watu ambao hawamfahamu jina lake lilikuwa ni zaidi ya tusi! "Naitwa Feri!" Akajibu kwa kifupi akiwa mwingi wa jazba. "Mtemi" huyu alijibu kinyonge. "Safi sana! Enhe...sasa nadhani tuwekane sawa hapa. Bwana Feri na Mtemi. Sisi tubahaidi kuwa rafiki wema sana kwenu kama tu mkitujibu tunachokitaka na mkatoa ushirikiano wa asilimia mia moja!" Huyu bwana akatamka uso wake ukikusanya hisia mchanganyiko za hasira na chuki. Kisha akasimama na kuwasogelea taratibu, "Ni wapi alipojificha Franko Dario?! Na shamba lake la hela liko wapi. Mkituambia haya mtatoka hapa kama raia huru wa nchi yenu huru, Tanzania!" Mtemi akanyanyua uso wake taratibu na kumtazama Feruzi. Akakutana na macho yanayouliza 'tuseme au tusiseme?'. Kimya kifupi kikapita... ******* Unyevu nyevu uliobeba ubaridi vikashirikiana kwa pamoja kumzindua baada ya kuzirai kwa muda ambao hakuweza kuukadiria. Ngozi ikaitika baada ya kugundua kuwa sehemu aliyopo ni kama amelowekwa ndani ya maji. "Ebooh nini tena!" Akashangaa. Macho yakaungana na ngozi yake iliyopigwa na upeo wa usiku unaokera. Akagundua kuwa amelala kwenye ufukwe na mawimbi ya maji yanayokuja na kuondoka yalikuwa yakifurahia kumlowanisha. "Ayaaa!" Akasimama upesi. Akaangaza huku na kule kama kuna mtu karibu, hakumuona. "Ina maana nimelala hapa ziwani au?" Akajishika paji lake la uso na mara moja akayakumbuka matukio yaliyomkuta mpaka akakutana na kiumbe cha kutisha. "Jini!" Akatamka. Anga la usiku huu lilinyimwa nuru ya mbalamwezi. Na kwa makadirio yake akapima kuwa ule ni usiku wa manane. Aende wapi? Akajipekua na hakuwa na simu zake zote. "Leo nimepatikana!" Akajisemea. Kwa mbali akaona umbo kubwa kiasi la mtu aliyekaa akichezea kitu kama mwangaza wa simu ndogo . Akatulia na kukaza macho yake kwenye giza lile. Akagundua kuwa huenda yule ni mvuvi au mlinzi wa eneo hili la beach akaamua kumsogelea ili aombe msaada wa haraka. Lahaula! Mtu yule alifanana kila kitu na yule kiumbe jini mtu aliyekutana naye usiku huu. Kabla hajachukua maamuzi yoyote yale ya kukimbia au kupiga mayowe mtu akammulika na tochi ya simu ile kisha akapaza sauti, "Njoo uchukue vitu vyako bwana! Mie sina kazi navyo." Hofu ikampotea ghafla na akasogea kwa unyonge. "Kaa hapa!" Akaamrishwa. "Uzembe ulioufanya tuliutarajia...na kwa bahati nzuri sana wewe sio mmoja wao hao waliomteka. Ama sivyo ningekufanya chakula cha samaki leo." Sauti yake nzito ikakoroma. "Sitaki ujue mambo mengi...uliyoyajua yanakutosha kama ukiongeza mengine utaingia matatani. Haya chukua simu zako na yote yaliyotendeka hapa yabaki kuwa siri. Ukiyapeleka kwingine utapotea!" Akamaliza na kusimama, Umbo lake kubwa lilimtisha sana Abednego. "Kaka samahani...kwani we ndiye uliagizwa kuja kumchukua Feruzi au?" Aliuliza swali kwa woga. "Naitwa Dubu! Feruzi ametekwa na mshukuru Mungu wako nimekuacha unaishi!" Mtu huyu akaondoka na kupotea eneo hili. Majibu magumu dhidi ya swali jepesi. Abednego hakuona usalama kuendelea kukaa eneo lile. Akaamua kuichangamsha miguu yake kukimbia kadri ilivyoweza kumbeba. Akakatiza barabarani kwa kasi nguo zake nzito zilizolowana zikamfanya mzito, akawaza kuzivua. Akaanza kwanza kutelekeza koti lake, kisha akatoa suruali ile kwa kuondoa mguu mmoja tu, Mara paap! Gari la doria hili hapa. Akamulikwa na taa zenye macho makali yanayotema mwanga mkali mno. Kwa woga akaanza kukimbia huku mguu mmoja wa suruali uko nje na mwingine umevaliwa. "Aisee yule nani yule?! Sio Kagoye yule?" Askari mmoja akauliza kwa shari. "Ni yeye aisee...halafu mbona kama kalowana, hebu tumkamate haraka!" Mwingine akadakia kwa ushabiki. Mbio za miguu ya mwanadamu hazijawahi kufua dafu mbele ya matairi ya gari. Abednego akiwa kama kichekesho akaangukia kwenye mikono ya wabaya wake kwa mara nyingine. Akiwa vilevile anayetetemeka kwa baridi na unyonge, wakampeleka moja kwa moja mpaka kwenye chumba alichokizoea, chumba chenye giza na harufu za ajabu ajabu ambazo ziliwafukuza mpaka nzi na mende. Rumande! Wakamkebehi huku wakimcheka kuwa hawataacha kumuandama mpaka aache uhalifu na biashara za magendo. Maswali aliyoulizwa hakuweza kujibu hata moja, Kwa nini anazurua usiku tena kwenye maeneo yaliyokatazwa? Kwa nini amelowana namna ile? Na kama hana makosa ni kwa nini amekimbia haraka baada ya kumulikwa na gari la doria maarufu kama tenga?! Wakaenda mbali na kumuuliza ile simu ya pili kaitoa wapi na wakati wamemzoea kuwa na simu ile moja tu wanayoifahamu? Ni Abednego Kagoye dhidi ya watesi wake wa siku zote. Hii vita yao, sisi hatuingilii. Usiku huu amekamatwa muda mbovu, muda wa majini, muda wa Dubu! ---------------------------- Mambo ni moto! Utamu kolea.... Huku wakisondekwa kwenyw kumbi za mahojiano. Kule wanasondekwa rumande. Umewahi kwenda rumande? Nyie kazi yenu ni ileile, Kuacha reaction zenu na kutoa maoni kwenye 0763204351. Maoni ni muhimu sana kwa mwandishi....kukosoa, kupongeza au kutoa zawadi πŸ˜ƒ. Tungeendelea KESHO...kama reaction zikifika 10. Kazi kwenu!

❀️ πŸ‘ πŸ‘ 😒 πŸ™ πŸ₯° 11
Image
Link copied to clipboard!